Quantcast
Channel: Swahili Net
Viewing all 28 articles
Browse latest View live

Kuyafanya Meno Yenye Rangi kuwa Meupe (Teeth Whitening)

$
0
0
Kuyafanya Meno Yenye Rangi kuwa Meupe

Wakati wa muongo uliopita mahitaji ya kuboresha muonekano au kurembesha meno yameongezeka kwa kiwango kikubwa hasa katika nchi zilizoendelea. Hii imechochewa na kupatikana kemikali mpya za meno (dental meterials) na vifaa kwa kasi ikiendana na kuboresha vile vya zamani. Sehemu nyingine iliyosababisha madaktari na mainjinia wa meno kuyafanya meno kuwa meupe ni sehemu ya fani ya taaluma ya meno chini ya urembeshaji wa meno, fani hii uhusika na kuboresha muonekano wa meno hasa yale yanayoonekana wakati wa kutabasamu na kuongea. Inahusisha matibabu kama kuyafanya meno yenye rangi kuwa meupe, kunyoosha meno yaliyojipanga vibaya pamoja na kukarabati meno yaliyovunjika na yale yaliyoumbika visivyo (malformed teeth). Huko Uingereza na sehemu nyingine za magharibi wanawake walio wengi wanatumia maelfu ya paundi/euro kuboresha muonekano wa meno yao hali ambayo inaanza pia kuingia huku kwetu.

Nini husababisha meno kugeuka rangi?
Meno kugeuka rangi husababishwa na kimojwapo au muunganiko wa vitu vifutavyo: -

  1. Vyakula na vinywaji kama vile vinyaji vyenye kaboni, wine na sigara.
  2. Utumiaji wa maji yenye kiwango cha juu cha madini aina ya magadi (fluoride) na utumiaji wa magadi katika kulainisha vyakula wakati wa kuandaa vyakula vigumu kama maharage na makande. Utafiti uliofanywa na Prof. Mabelya na wenzake nchini Tanzania umeonesha kuwa kubadilika kwa rangi ya meno kutokana na magadi kwa kiwango kikubwa husababishwa na matumizi ya magadi katika mapishi ya vyakula hasa makande kule maeneo ya mkoa wa Kilimanjaro/Moshi kuliko inavosababishwa na matumizi ya maji.
  3. Maumbile yasiyo sahihi ya sehemu ngumu za jino (enamel and dentine defects). Iwapo sehemu ngumu ya meno imeumbwa ikiwa laini ni rahisi kufyonza rangi na jino kuota likiwa limegeuka rangi au kubadilika baada ya kuota.
  4. Matumizi ya madawa kwa mama mjamzito ambaye tayari meno ya mtoto aliye tumboni yameanza kuumbwa lakini hayajapata madini ya kutosha na hata watoto wachanga ambao meno yao hayajakomaa.
  5. Kufa kwa kiini cha jino hasa kutoka na kujigonga wakati wa ajali au kupigana ngumi usoni (pulp necrosis), jino likigongwa kwa nguvu damu huvuja ndani ya kiini cha jino na baadaye huchachuliwa na kutoa kemikali ambayo hupenya kwenye vitundu vidogo vidogo kwenye dentine na kujidhihirisha kama kijivu, zambarau au hata nyeusi. Hali hii yaweza tokea mapema baada ya kupata ajali lakini wakati mwingine inaweza kuchukua miaka kadhaa hata arobaini kipindi ambapo mtu hakumbuki kuwa aliwahi kutwangwa ngumi.

Kuyafanya meno yenye rangi yasimpendeza mwenye nayo kuwa meupe
(Bleaching or teeth whitening)

Huku ni kuyafanya meno yen
ye rangi kuwa meupe au kuongeza weupe wa yale yenye rangi ya kawaida kufikia kiwango cha weupe atakacho muhitaji kwa kutumia kemikali maalum. Rangi ya kawaida ya meno kwa walio wengi ni uweupe kama wa maziwa (milky white). Rangi yeyote nje ya hiyo si ya kawaida (abnormal color or discoloration).

Kuwa na rangi isiyo ya kwaida hasa kwa meno ya mbele linaweza kuwa tatizo kubwa la urembo na kumsumbua mhusika kisaikolojia. Kuyafanya meno kuwa meupe kumelenga kuwaondolea wahusika tatizo hili japo mafanikio yake yanategemea kiwango cha rangi isiyo ya kawaida.

Kufanya meno kuwa meupe kwa kutumia kemikali, kunaweza kubadili yaliyo na rangi isiyo ya kawaida kutoka yale yaliyoathirika kwa kiwango kidogo mpaka cha kati.

Kufanya meno yawe meupe kwa kutumia kemikali huunguza (oxidises) rangi ya jino na kuiondoa. Kemikali zinazotumika zina hydrogen peroxide 30%-35% na baadhi carbamide peroxide 10%. Kemikali hizi huweza kuondoa rangi zilizosababishwa na vyakula, vinywaji, dawa za tetracycline, rangi kidogo iliyotokana na utumiaji wa madini ya magadi kwenye vyakula au kwenye maji (mild fluorosis) na meno yenye rangi ya njano au kijivu itokanayo na umri kuwa mkubwa. Inaweza pia kuondoa rangi itokanayo na uvutaji wa sigara na matumizi ya ugoro. Kwa wavutaji wa sigara sharti waache pindi watumiapo kemikali hizi kwani muunganiko wa hydrogen peroxide na kemikali zilizopo kwenye moshi wa sigara unahisiwa kuongeza madhara zaidi ambayo tayari moshi wa sigara husababisha kwenye mwili wa binadamu. Haishauriwi kwa akina mama wanaonyonyesha kutumia dawa hizi pamoja na kwamba hakuna madhara yanayojulikana mpaka sasa


Kupiga meno viraka (Veneeri
ng)


Kupiga meno viraka



Hii hufanyika kwa kuondoa sehemu ndogo ya juu ya jino kwenye enamel kama 0.5-1mm na baadaye kupandika dawa yenye rangi nyeupe kulingana na mgonjwa anavyotaka mwenyewe. Picha inayonesha meno yaliyobadlika rangi kutokana na magadi kabla na baada ya kupigwa viraka


Kabla ya kiraka Baada ya kupigwa kiraka (veneer)

Kumbuka: kuna rangi zaidi ya 26 nyeupe ambazo miongoni mwake mgonjwa anaweza kuchagua anayoitaka

Unyongovu Waweza Kusababisha Magonjwa ya Moyo kwa Vijana

$
0
0
jaribio la kujiua

Katika tafiti mpya zilizofanywa hivi karibuni zinaonyesha kuwa unyongovu na jaribio la kujiua ni viashiria hatari ambavyo huleteleza vijana kufa kwa magonjwa ya moyo.

Katika utafiti mkubwa uliohusisha washiriki zaidi ya 7000 walio chini ya miaka 40 ulionyesha kuwa kwa wale waliokuwa na historia ya unyongovu au jaribio la kujiua walikuwa na hatari kubwa zaidi ya kufa kutokana na magonjwa ya moyo hasa yale ambayo moyo hukosa oksijeni ya kutosha (ischemic heart disease) ukilinganisha na wale ambao hawakuwa na historia hiyo.

Ingawa jinsia zote zilikuwa kwenye hatari zaidi ya kufa kutokana na magonjwa ya moyo, lakini wanawake wenye unyongovu au waliofanya jaribio la kujiua walikuwa na hatari mara 14 zaidi ya kufa kwa magonjwa ya moyo yatokanayo na kukosa oksijeni ya kutosha (ischemic heart disease) kulinganisha na wale ambao hawakuwa na unyongovu au jaribio la kujiua.

Katika utafiti huu uliofanywa na Profesa Viola Vaccarino kutoka chuo kikuu cha Emory, Atlanta, Georgia aligundua jinsi matatizo ya kisaikolojia yanavyopelekea kuongeza hatari ya kufa mapema na magonjwa ya moyo katika idadi ya vijana.

Taarifa nyingi zilizopo za magonjwa ya moyo ambazo zilizokwisha tolewa huwa za umri wa kati na wazee, maana imekuwa ikizoeleka magonjwa haya huathiri zaidi rika hiyo, ambayo ni kweli kabisa hasa katika magonjwa yanao athiri zaidi mishipa ya damu ya moyo (CHD).

Kutokana na watatifi mkazo humewekwa zaidi kwa wazee ingawa magonjwa mengi ya moyo huanza katika kipindi cha ujanani.

Katika utafiti huu taarifa zilichukuliwa kutoka kwa washiriki 7641, wenye umri kati ya 17 hadi 34, kutoka mwaka 1988 hadi 1994.

Katika ratiba ya uchunguzi, tathmini ilikuwa kuhusu unyongovu na jaribio la kujiua , na matokeo baada ya ufuatiliaji yalikuwa kama ifuatavyo: washiriki 51 walikufa kutokana na magonjwa ya moyo, na kati ya hao 28 walikufa kutokana na moyo hukosa oksijeni ya kutosha (ischemic heart disease).

Wagonjwa 538 walikutwa na historia ya unyongovu na 419 kuwa na jaribio la kujiua. Na 136 walikuwa na historia ya vyote viwili.

kubadilishwa athari ya uwiano (HR) kwa ajili ya hatari kwa CVD kifo 2.38 kwa ajili ya wagonjwa walio na unyogovu (95% ya muda kujiamini [CI], 0.93-6.08) na 3.21 kwa ajili ya wale walio na majaribio ya kujiua zamani (95% CI, 1.36-7.56)

Kuna mjadala mkubwa kuhusu madhara ya unyogovu na ugonjwa wa moyo na mishipa katika vifo vya wanawake kama ikilinganishwa na wanaume. Nadhani ushahidi kutoka kwa utafiti huu ni imara lakini masomo ya baadaye ni wazi kuwa ni muhimu.

Mmoja wa watafiti wengine Dr Scherrer alisema “kwa madaktari, anadhani matokeo ya jumla yanazidi kuongeza wasiwasi ni wakati gani hutambua unyongovu, ambapo ni kawaida kwa watu wenye umri mdogo, kuna uwezekano wa haja ya kuweka mkazo mkubwa katika kufuatilia afya yao ya moyo. Na kwamba sio kitu ambacho madaktari wengi hufanya mara kwa mara kwa wagonjwa wenye umri mdogo sana.

Na hii huacha swali kubwa la kujiuliza:

Je inawezekana kuzuia magonjwa ya moyo yahusishwayo na unyongovu, kwa kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa mambo ya hatari yanayoweza kupelekea magonjwa ya moyo kwa kundi la vijana?

Kuoza kwa Kasi kwa Meno Mengi kwa Watoto Wadogo (Rampant Caries in Children)

$
0
0
Rampant Caries in Children-kuoza kwa meno watoto

Tafsiri za maneno “rampant caries” ni nyingi katika fani ya meno lakini la msingi ni kuoza kwa meno kunako enea kwa kasi na kuharibu vichwa (crowns) vya meno mengi au yote yaliyoota. Hii ni hali mbaya ya kuoza kwa meno ambayo hushambulia zaidi meno ya utotoni (milk teeth or primary dentition), japo wakati mwingine hata ukubwani.

Ugonjwa huu unajidhihirisha kwa kuanza na kuongezeka kwa kasi na kwa namna unavyo yashambulia meno na vyanzo vyake. Meno hushambuliwa kwa mpigo hasa kuanzia meno ya juu mbele, ingawa meno ya chini mbele ni mara chache kushambuliwa kwa vile yanakingwa na visababisha vya kuoza na ulimi.

Ugonjwa huu hushambulia hata maeneo ya meno ambayo kwa hali ya kawaida si rahisi kuoza, kama sehemu ya kukatia kwa meno ya mbele (incisal edges) na sehemu ya mbele kati na nyuma kati (facial and lingual surfaces).

Nini husababisha meno kuoza kwa kasi utotoni?

Nadharia nyingi zinaonesha kuna uhusiano mkubwa kati ya ugonjwa huu na tabia ya ulaji ya mtoto (feeding habits). Mfano kisababishi kikubwa ni watoto kunywa vinywaji vyenye sukari kwa muda mrefu na mara nyingi kwa kutumia chupa za kunyonyea (nursing bottles) ndiyo maana ugonjwa huu wakati mwingine huitwa nursing bottle caries. Hii hujitokeza hasa kwa watoto wanaochwa na yaya zao, ambao huwapa vinywaji hivyo kila wanapohitaji au wakilia.

Pamoja na kwamba ugonjwa huu hutokana zaidi na chupa za kunyonyea, japo mara chache, lakini pia yawezekana kutokana na mama kumnyonyesha mtoto mara kwa mara au tuseme kila anapo hitaji; vile vile wale akina mama ambao hawataki usumbufu usiku hivyo kutumbukiza nyonyo zao kwenye vinywa vya watoto na wao kujilalia, hapa mtoto hujinyonyea usiku kucha hali hii kitaalamu hujulikana kama at will breast feeding.

Vijino vilivyoathirika huonekana brauni au vyeusi kama mkaa

Watoto walio katika hatari ya kupata ugonjwa huu

  • Watoto wa masikini ambao hawapigi mswaki kwa kizingizio cha kwamba mtoto ni mdogo, kumbuka meno ya utotoni yana madini kidogo
  • Watoto wa wafanyakazi wanashinda maofisini wakati wa kunyonyesha na waacha watoto kutumia chupa za kufyonzea kwa muda mrefu ambao hawapo nao
  • Watoto wagonjwa sugu wanaotumia dawa zenye sukari (syrups) mara kwa mara.
  • Watoto wanaoachwa kunyonyeshwa mapema na hivyo kutumia chupa kama mbadala

Namna ya kumkinga mtoto wako

  • Punguza matumizi ya chupa za kufyonzea
  • Msipende kuwanyonyesha watoto kila wanapotaka hivyo, hasa kunyonyesha inapotumika kama njia ya kupoza mtoto anayelia
  • Jenga tabia ya kuwakagua watoto vinywani mara kwa mara na ukiona tatizo mpeleke hospitali mapema
  • Wasaidieni watoto kupiga mswaki mara baada ya meno kuanza kuota
  • Dhibiti matumizi ya vinywaji na na vitu vya sukari mara kwa mara
  • Msipende kuwapa watoto wadogo fedha kwani matumizi yake ni pipi na ice water au vinavyo fanana na hivyo

Matibabu

  • Kuziba meno yanayoweza kuzibika
  • N’goa yanayouma na hayawezi kuzibika na kutumia vitunza nafasi (space maintainers).
  • Acha yasiyoweza kuzibika lakini hayaumi yatatoka wakati wake ukifika
  • Pakaza madini ya fluorini kwa watoto walio katika hatari kubwa

Upandikizaji wa seli za mfumo wa fahamu waweza kutibu kisukari

$
0
0

Watafiti nchini Japan wamegundua jinsi seli za mfumo wa fahamu zinavyoweza kutumika kama seli mbadala zinazofaa kupandikizwa kwenye seli kongosho ili kutibu kisukari. Ripoti ya utafiti huo ambayo imechapishwa kwenye jarida la kitafiti la EMBO Molecular Medicine, inaonesha kuwa seli zinazovunwa kutoka katika mfumo wa fahamu zinaweza kupandikizwa katika tezi kongosho na hivyo kumaliza tatizo la ukosefu wa seli za beta ambazo huitajika kwa ajili ya uzalishaji wa insulin.

Kisukari ni ugonjwa unaosababishwa na ukosefu wa kichocheo cha insulin kinachozalishwa na tezi kongosho, na ambao huathiri karibu watu milioni 200 duniani. Mpaka sasa hakuna tiba yeyote ya ugonjwa huu, hali inayowafanya wagonjwa wa kisukari kutegemea zaidi matumizi ya dawa au njia nyingine mbadala kuthibiti kiwango cha sukari mwilini.

Utafiti huo ulioongozwa na Dr Tomoko Kuwabara kutoka taasisi ya tafiti za Afya ya AIST ya Tsukuba nchini Japan, ulilenga katika kuchunguza jinsi seli za binadamu zinavyokua na kijiwagawa kulingana na kazi mbalimbali za mwili, na pia kuchunguza uwezekano wa kutumia seli mbalimbali kutekeleza kazi zilizo nje ya majukumu yake ya kawaida.

Katika kufafanua, Dr. Kubawara anasema kuwa kwa vile kisukari ni ugonjwa unaosababishwa na ukosefu wa aina moja ya seli, ugonjwa huu unaweza kutibika kwa kutumia njia ya upandikizaji wa seli mpya zitakazotumika kuzalisha kichocheo cha insulin. Anasema, hata hivyo kwa vile kupandikiza seli za beta kutoka tezi kongosho za watu wengine ni ngumu kwa sababu ya ukosefu wa watoaji, njia muafaka ni kutumia seli za mfumo wa fahamu wa mgonjwa mwenyewe katika kufanikisha upandikizaji huo.

Seli za mfumo wa fahamu zinazoweza kupandikizwa kwenye tezi kongosho kwa urahisi zaidi ni zile zilizopo katika maeneo ya ubongo wa mbele yajulikanayo kitaalamu kama hippocampus na olfactory bulb.

Kwa kawaida seli za mfumo wa fahamu huzalisha kiwango kidogo sana cha insulin tofauti na seli za tezi kongosho, hata hivyo, mara tu baada ya kupandikizwa kwenye tezi kongosho, seli hizo zilianza kutoa kiwango kikubwa cha kichocheo cha insulin na kiwango cha sukari katika damu kilionekana kupungua kwa kiwango kikubwa. Na hata seli zilizopandikizwa zilipoondolewa, kiwango cha insulin kilishuka na kusababisha kupanda tena kwa kiwango cha sukari katika damu.

Utafiti huo ulifanyika kwa kutumia panya waliokuwa na ugonjwa wa kisukari.

Upandikizaji uliofanywa katika majaribio haya wa seli za mfumo wa fahamu kwenda kwenye tezi kongosho, siyo tu umeonesha uwezo wa seli za mfumo wa fahamu kuthibiti uzalishaji wa kichocheo cha insulin, bali pia ukweli kuwa seli zinazotajika kwa ajili ya upandikizaji zinaweza kutoka kwa mgonjwa mwenyewe bila kuhitaji uwepo wa mtoaji (donor).

Akihitimisha, Dr. Kubawara alisema kuwa, matokeo ya utafiti wao yameonesha uwezo mkubwa wa seli za mfumo wa fahamu katika kutibu kisukari bila kuhitaji kufanya mabadiliko ya kinasaba au mtoaji (donor), hali ambayo inaleta matumaini ya kuondokana na tatizo la ukosefu wa watoaji wa seli za upandikizaji siku za mbele.

Dawa za Usingizi Chanzo cha Saratani na Kifo

$
0
0
Dawa za Usingizi
Utafiti uliofanywa nchini Marekani hivi karibuni umetoa matokeo ya kushangaza kwa kusema ya kwamba matumizi ya dawa za usingizi huongeza hatari ya kupata saratani pamoja na mtu kufa mapema. Utafiti huo umesema wale wanaotumia dozi kubwa ya dawa ya usingizi wako kwenye hatari ya kupata magonjwa ya saratani.
Utafiti huo ambao ulifanywa na watafiti wa kitengo cha usingizi katika kituo cha Jackson Hole Centre for Preventive Medicine in Wyoming and the Scripps Clinic Viterbi Family Sleep Centre kilichopo jijini California nchini Marekani ili kuangalia hatima ya watu wanaotumia dawa za usingizi aina ya benzodiazepines kama temazepam, diazepam (valium), dawa mpya aina ya zolpidem, zopiclone, zaleplon, dawa za jamii ya barbiturates na zile zinazotumiwa kutibu mcharuko mwili (allergy) na ambazo huleta usingizi.
Matokeo ya utafiti huo yanasema wale wanaotumia dawa za usingizi (Hypnotics) walizoandikiwa na Daktari wako kwenye hatari ya 4.6 kufa ndani ya miaka 2 na nusu ukilinganisha na watu ambao hawatumii dawa za usingizi. Wale ambao wanatumia dozi ndogo ya dawa za usingizi yaani wanaotumia wastani wa vidonge 4-18 kwa mwaka wako kwenye hatari ya mara 3.6 zaidi kufa kulinganisha na wale ambao hawatumii dawa za usingizi.
Wale wanaotumia dozi kubwa yaani vidonge 18-132 kwa mwaka wako kwenye hatari kubwa ya mara 4.4 zaidi kufa, na wale wanaotumia zaidi ya vidonge 132 kwa mwaka wako kwenye hatari ya mara 5.3 zaidi kufa kulinganisha na wale ambao hawatumii dawa za usingizi. Asilimia 93 ya wale walioshiriki katika utafiti huu walikuwa ni wale wanaotumia dozi kubwa ya dawa za usingizi. Pia wale wanaotumia dozi kubwa ya dawa hizi wako kwenye hatari ya asilimia 35 kupata saratani kubwa. Kwa wale wanaotumia dawa aina ya zolpidem wako kwenye hatari ya mara 5.7 kufa huku wale wanaotumia dawa aina ya temazepam wako kwenye hatari ya mara 6.7 kufa kulinganisha na wale wasiotumia dawa za usingizi.
Utafiti huo umesema wale walio kwenye hatari ya madhara haya ya dawa za usingizi ni wale walio katika umri wa miaka 18-55 ingawa sababu halisi haikuelezwa katika matokeo ya utafiti huo. Wagonjwa 10,500 wanaotumia dawa za usingizi walishiriki katika utafiti huo wakilinganishwa na watu 23,500 ambao hawatumii dawa za usingizi walioshiriki katika utafiti huo.
Watafiti hao walisema tiba ya kutotumia dawa yaani ya tiba ya utambuzi wa tabia (cognitive behavior therapy) inaweza kuwa na manufaa zaidi kuliko matumizi ya dawa za usingizi na hata matumizi ya dawa za usingizi kwa muda mfupi yanapaswa kuangaliwa kwa makini. Watafiti hao wakiandika katika jarida la British Medical Journal walisema “Faida chache zinazopatikana kutokana na matumizi ya dawa za usingizi ambazo zilitafitiwa kwa kina na makundi ambayo hayana maslahi yoyote na dawa hizi haziwezi kuhalalisha madhara yatokanayo na matumizi ya dawa hizi za usingizi”.
Matokeo ya utafiti huu ni changamoto kubwa katika fani ya afya hasa ukizingatia ya kwamba watu wengi hutumia dawa za usingizi kutokana na kupatikana kiurahisi katika maduka mbalimbali ya dawa katika Afrika Mashariki. Pia ni changamoto kubwa sana kutokana na dawa hizi kutumika wakati wa upasuaji, kutibu magonjwa ya akili, kutibu mcharuko mwili, msongo wa mawazo na hata kwa wazee.
Kulingana na matokeo haya ni vizuri kuangalia upya matumizi ya dawa za usingizi na utafiti zaidi unahitajika kufanyika kabla ya kutoa msimamo kuhusu matumizi ya dawa za usingizi.

Machungwa, Zabibu Hupunguza Uwezekano wa Kupata Kiharusi

$
0
0
zabibu
machungwa
Utafiti mpya uliofanyika nchini Marekani umesema ya kwamba kula machungwa na zabibu kunaweza kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi (Stroke).
Utafiti huo uliangalia faida za matunda chachu (Citrus Fruit) pekee kwa mara ya kwanza tofauti na tafiti nyingi ambazo tumezizoea zinazoangalia umuhimu wa matunda na mboga za majani kwa afya kiujumla.
Utafiti huu umehusisha maelfu ya wanawake wanaoshiriki katika tafiti ya manesi Nurse’s Health Study lakini wataalamu wanaamini faida hizo za machungwa na zabibu pia zinapatikana kwa wanaume.
Timu ya watafiti katika chuo cha Norwich Medical School katika Chuo Kikuu cha East Anglia wamechunguza umuhimu wa kemikali aina ya flavonoids ambayo ni jamii ya antioxidant (kemikali zinauwa kemikali hatari za kwenye mwili) inayopatikana katika matunda, mboga za majani, chocolate nyeusi na wine nyekundu.
Utafiti huu ulifuatilia takwimu za miaka 14 za wanawake 69,222 ambao walikuwa wakishirki katika tafiti kwa kuandika kiwango chao cha kula matunda na mboga za majani kwa kila kipindi cha miaka 4. Timu hiyo ya utafiti iliangalia uhusiano wa aina sita ya flavonoids - flavanones, anthocyanins, flavan-3-ols, flavonoid polymers, flavonols na flavones na hatari ya aina mbalimbali za kiharusi kama Ischaemic, Hemorrhagic na Total Stroke. Ilionekna wanawake waliokula kiwango kikubwa cha flavanones kwenye matunda chachu walikuwa na asilimia 19 ya uwezekano wa kupunguza kiharusi kulinganisha na wanawake ambao walikula kiwango kidogo cha matunda hayo.
Kiwango kikubwa cha flavanones kilikuwa 45mg kwa siku kulinganisha na kiwango kidogo cha 25mg kwa siku. Utafiti huu ulichapishwa katika jarida la Medical Journal Stroke umesema flavanones hupatikana kwa asilimia 82 kwenye machungwa na juisi ya machungwa na hupatikana kwa asilimia 14 kwenye zabibu na juisi ya zabibu. Hata hivyo watafiti hao wamesema kwa wale wenye kusudio la kuongeza kiwango kikubwa cha flavanones itawalazimu kula tunda la chungwa kwa wingi na si juisi za machungwa zinazotengenezwa kiwandani kutokana na kiwango kikubwa cha sukari kinachopatikana katika juisi hizo za viwandani.
Professa Aedin Cassidy wa masuala ya lishe bora (nutrition) na ambaye alikuwa kiongozi wa utafiti huo amesema “kula kwa wingi kwa matunda, mboga za majani, na hasa Vitamin C uhusishwa na kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi”. Flavanones hutoa kinga dhidhi ya kiharusi kutokana na kuongeza ufanisi wa mishipa ya damu kwenye ubongo na kutokana na kuwa na uwezo wa kuzuia maambukizi mwilini (Anti-inflammatory effect).
Utafiti uliofanyika hapo awali ulionyesha ya kwamba ulaji wa matunda chachu na juisi yake na si matunda ya aina nyingine yoyote hupunguza uwezekano wa kupata kiharusi aina ya Ischaemic Stroke na kuvuja damu kwenye ubongo (Intracerebral Haemorrhage).

Utafiti mwingine uliofanyika kipindi cha nyuma ulionyesha hakuna uhusiano wowote wa matunda ya njano na machungwa katika kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi lakini ulionyesha ya kwamba kuna uhusiano wa zabibu na mapeasi wa kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi.
Katika utafiti mwingine uliofanyika nchini Sweden umeonyesha ya kwamba wanawake ambao walikula kiwango kikubwa cha antioxidant karibia asilimia 50 kutoka kwenye matunda na mboga za majani, ni wachache tu kati yao waliopata kiharusi ikilinganishwa na wanawake ambao walikuwa na kiwango kidogo cha antioxidant.
Matokeo ya utafiti huu yasiwafanye watu kuacha kula matunda ya aina nyingine pamoja na mboga za majani kwani nayo yana faida kubwa katika mwili wa binadamu.
Kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi inawezekana kama mtu atakula lishe bora iliyo na virutubisho vyote muhimu, kula matunda na mboga za majani kwa wingi, kufanya mazoezi mara kwa mara, kupunguza kiwango cha ulaji chumvi (kwani watu wenye asili ya Kiafrika wana kiashiria cha asili kinachojulikana kama salt retention gene ambacho hufanya kiwango kidogo cha matumizi ya chumvi mwilini kuonekana kama kiwango kikubwa na hivyo kuongeza hatari ya kupata kiharusi), kupunguza uzito (kuwa kwenye uzito unaotakikana kiafya kulingana na umri na urefu wako), kupunguza kiwango cha matumizi ya mafuta katika chakula, kulala masaa ya kutosha na kupunguza msongo wa mawazo.

Jinsi ya Kuandaa Chakula cha Mtoto

$
0
0
 Chakula cha Mtoto

Mtoto ale chakula muda gani?

Chai ya asubuhi: Saa 12:00 mpaka 2:00 kutegemeana na ni muda gani mtoto anakwenda shule. Jambo la muhimu ni kuwa, mzazi/mlezi ahakikishe mtoto anakula asubuhi ili asiende shle akiwa na njaa, ikibidi mzazi/mlezi amfungie mtoto chakula abebe.

Chakula cha mchana: Muda wa kati ya saa 5:30 mpaka saa 7:00 mchana.

Chakula cha jioni: Saa 10:00

Chakula cha usiku: Saa 1:00 usiku

Jinsi ya kuandaa chakula cha siku ya Jumatatu

Asubuhi: Kifungua kinywa (Breakfast)

Mlo 1: Chapati Maji Na Juisi Ya Chungwa

Mahitaji: 250 gram Unga wa ngano, 1 yai, 100 gram maziwa ya maji, 20 gram mafuta ya mahindi, 10 gram baking powder

Jinsi ya kuandaa chapati maji: Changanya vitu vyote katika bakuli kisha piga na mchapo mpaka upate mchanganyiko safi na laini kabisa. Iwapo mchanganyiko bado mzito ongeza maji kiasi.

Jinsi ya kuandaa juisi ya chungwa: Menya chungwa safi kabisa ili kuondoa uchungu wa gesi iliyopo katika maganda. Kisha tumia chombo maalumu cha kukamulia juice, kamua kisha hifadhi katika friji bila kuweka sukari ili ikae kwa muda bila kuharibika. Kumbuka pia kuweka sukari wakati wa kunywa.

Mlo 2: Uji wa Ulezi na Mtindi

Mahitaji: 200 gram unga wa ulezi, 100 gram maziwa ya maji, 350 gram maji, 100 gram mtindi usio na ladha ya matunda

Jinsi ya kuandaa uji wa ulzei na mtindi: Changanya unga wa ulezi na maziwa katika bakuli kisha chukua sufuria weka maji kiasi cha gram 350. Chemsha maji yakishachemka weka mchanganyiko wa maziwa na unga wa ulezi koroga mpaka uchemke na kuchanganyika safi kabisa ili uji wako usishike chini na kuungua. Acha uchemke vizuri kisha onja ukipata ladha ya kuiva kwa nafaka utakua tayari.

Toa jikoni weka katika bakuli litakalotumiwa na mtoto kisha changanya mtindi usio na ladha ya matunda pamoja na sukari tayari kwa mtoto kunywa.

Mchana: Chakula cha mchana

Mlo: Glass ya maziwa na mkate wa nyama za kusindika

Jinsi ya kuandaa: Mpatie mtoto 200 gram za maziwa sawa na glasi moja ya uvuguvugu au ya baridi lakini kumbuka yawe yamechemshwa vizuri na yakapoa kwa ajili ya usalama.

Kisha chukua vipande viwili vya mkate paka siagi au mayonaisi. Kisha chukua beef salami na beef backon weka kati kati pamoja na slice ya nyanya na tango mbichi mpatie mtoto ale.

Jioni: Chakula cha jioni

Mlo: Sahani ya mchanganyiko wa mboga mbichi

Jinsi ya kuandaa: Chukua caroti, tango, pilipili hoho nyekundu na ya kijani zote mbichi na zuchini ichemshe kidogo kisha weka mtindi wenye ladha ya matunda kwa ajili ya kulia hizo mboga

Huu ndio muonekano wa sahani ya mchanganyiko wa mboga kama mtoto ni mdogo sana zisage kwenye mashine ya kusagia nyama kisha utapata mchanganyiko laini mpatie mtoto asiyeweza kutafuna hizo mboga mbichi.

Usiku: Chakula cha usiku

Mlo 1: Supu ya uyoga

Mahitaji: 300gram Uyoga fresh au wa kopo, 50 gram kitunguu maji, 10 gram kitunguu swaumu, 10 gram tangawizi, 50 gram leeks, 100 gram viazi mbatata, 100 gram maziwa fresh, 50 gram mafuta ya kupikia, 300 gram maji

Jinsi ya kuandaa supu ya uyoga: Kaanga katika mafuta ya kupikia vitunguu maji na vitunguu swaumu pamoja na tangawizi. Kisha weka viazi mbatata, leeks na uyoga kaanga tena kiasi kisha weka maziwa na maji acha ichemke mpaka viazi viive kisha toa na saga kwenye blenda. Rudisha jikoni kama itakuwa nzito sana ongeza maziwa au maji kiasi. Usisahau kuweka chumvi kulingana na ladha.

Mlo 2: Kuku maziwa, muhogo na njegere

Mahitaji: 200 gram nyama ya kuku isiyo na mifupa, 100 gram njegere, 200 gram maziwa, 150 mihogo iliyochemshwa kwanza, 300 gram maji

Kulia ni machine ya kusagia nyama utakayoitumia kwa ajili ya kusagia vyakula mbali mbali.

Jinsi ya kuandaa kuku maziwa, muhogo na njegere: Chemsha vyote kwa pamoja kuku na njegere mbichi pamoja na muhogo uliokwisha chemshwa kwanza mpaka ikaribie kukauka mchuzi kisha toa jikoni. Chuja kisha weka mchuzi pembeni.

Chukua mchanganyiko wa njegere, kuku na muhogo. Tumia machine ya kusagia nyama weka huo mchanganyiko kisha saga upate rojo zito kisha rudisha katika sufuri, changanya na ule mchuzi uliochuja ongeza chumvi kulingana na ladha mpe mtoto ale chakula kikiwa cha moto.

Kama huna mashine ya kusagia nyama tumia mwiko kuponda itakua safi kabisa kisha unachanganya na ule mchuzi uliochuja.

Kwa mtoto mkubwa usisage. Baada ya kuchemsha ikaiva ongeza chumvi kisha mpakulie ale chakula cha moto atafurahia sana mchanganyiko wa ladha ya chakula hiki.

Orodha kwa ajili ya manunuzi siku ya Jumatatu

Uyoga wa kopo au fresh, mihogo mibichi, pili pili hoho, tangawizi, unga wa ngano, mayai, maziwa, sukari, chumvi, njegere, nyama ya kuku, tango, zucchini, mtindi usio na ladha ya matunda, mtindi wa ladha ya matunda, baking powder, viazi mbatata, mafuta ya mahindi na leeks.

Vitu hivi vyote sio vingi na unaweza kuvitumia siku inayofuata maana menu yetu ina uwiano safi kabisa. Vitu vingi vinatumika karibu kila siku na manunuzi yake sio ghali kabisa. Mpe mwanao raha kwa kula chakula safi na salama.

Unene Uliopitiliza (Obesity)

$
0
0
Unene Uliopitiliza (Obesity)
Tatizo la Unene Uliopitiliza (Obesity)

Tatizo hili la unene uliopitiliza kuliko inavyohitajika kiafya huwa linaletwa na kuongezeka kwa kiwango cha mafuta mwilini. Njia rahisi na inayokubalika ya kuweza kugundua kama mtu ni mnene kupita kiasi (obese) inafahamika kama kipimo cha Body Mass Index (BMI). Vipimo hivi vya BMI ndio vinaweza kukujulisha kama unene ulionao unastahili kulingana na umri, urefu na uzito wako. Vipimo hivi ni kama ifuatavyo:

Jinsi ya kupima BMI yako

Kanuni ya BMI hutumia uzito wa mtu pamoja na urefu wake. Uzito wa mtu hupimwa katika kilograms (kg) na urefu wake katika mita (m) au sentimita (cm). Ikumbukwe pia kuwa mita moja ni sawa na sentimita 100 na mita² = mita x mita.

CategoryBMI range – kg/m2
Emaciationless than 14.9
Underweightfrom 15 to 18.4
Normalfrom 18.5 to 22.9
Overweightfrom 23 to 27.5
Obesefrom 27.6 to 40
Morbidly Obesegreater than 40

BMI (kg/m2) = Uzito katika kilograms/Urefu katika meters². Maana yake ni kwamba ili kuweza kupata BMI itakayokuwezesha kujifahamu kama u mnene ama la, chukua uzito wako gawa kwa kipeo cha pili cha urefu wako.

Tatizo la unene uliopitiliza husababishwa na nini ?

Kuna mambo kadhaa yanayoweza kusababisha unene uliopitiliza. Mambo hayo ni pamoja na

  • Vyakula vya mafuta - Ulaji wa vyakula venye mafuta mengi au calories nyingi.
  • Kutofanya mazoezi - Wale wasiofanya mazoezi mara kwa mara huwa wanene tofauti na wale wanaofanya mazoezi.
  • Kurithi viashiria vya asili (genes) - Viashiria hivi vinaweza kuwa moja ya vichocheo vya kuongeza uzito kwani ndivyo huamua wapi mafuta huhifadhiwa mwilini na kwa kiwango gani. Lakini haimanishi kuwa mtu akiwa navyo basi ndio atakumbwa na tatizo hili.
  • Umri - Watu wengi huongezeka uzito au hunenepa kadri umri unavyoongezeka kwa sababu wanakuwa hawajishughulishi sana (less active) na huwa wanapungua maumbile ya miili yao (muscles mass)
  • Matatizo ya kisaikolojia - Wakati mwengine watu wenye matatizo ya kisaikolojia au msongo wa mawazo (stress) huwa na tabia ya kula sana, matokeo yake ni kunenepa.
  • Dawa - Baadhi ya dawa zenye madhara ya kuongeza unene ni kama corticosteroids, blood pressure medications, tricyclic medications na kadhalika.
  • Matatizo ya afya - Baadhi ya magonjwa yanachangia kuongezeka kwa uzito au kenenepa kama cushings syndrome, hypothyroidism, osteoarthritis na kadhalika

Vihatarishi vya tatizo la unene wa kupitiliza

Aidha yapo mambo kadhaa ambayo yanaweza kumuhatarisha mtu kupata unene wa kupitiliza. Mambo haya ni pamoja na

  • Kukua kwa uchumi wa nchi - Wananchi wengi wanaoishi kwenye nchi zilizoendelea au wenye kipato kikubwa ndio wanaopata tatizo hili kutokana na kuishi mfumo wa maisha ya kivivu na hali ya kutokufanya mazoezi (sedentary lifestyle).
  • Historia ya kuongezeka uzito uliopitiliza kwenye familia nayo yaweza kuhatarisha mtu kupata tatizo hili. Aidha, si jambo la kushangaza kuona karibu familia nzima au wengi wa wanafamilia kuwa wanene kupitiliza.
  • Kutojishughulisha na chochote (inactive).
  • Kupenda kula sana kuliko kawaida (overeating).
  • Kula vyakula vya mafuta mengi
  • Kutumia dawa zenye madhara ya kuongeza uzito uliopitiliza.
  • Kuwa na ugonjwa wa vichocheo mwilini (hormonal disorders) kama cushingsyndrome, hypothyroidism.
  • Kuwa na msongo wa mawazo au kuathirika kisaikolojia.

Magonjwa yanaoweza kuambatana na tatizo la unene uliopitiliza

  • Kisukari
  • Shinikizo la damu (hypertension)
  • Kiharusi (Stroke)
  • Magonjwa ya moyo
  • Tatizo la kutopumua vizuri wakati mtu yupo usingizini (Sleep apnea)
  • Vijiwe katika mfuko wa nyongo (Gallstones)
  • Kiwango cha juu cha lijamu kwenye damu(cholesterol ikiwemo triglycerides)
  • Ugonjwa wa mifupa kama yabisi (osteoarthritis).
  • Saratani ya matiti
  • Saratani ya tezi dume (prostate cancer)
  • Saratani ya utumbo mpana pamoja na maeneo ya haja kubwa (Colorectal cancer)
  • Matatizo ya mzunguko na mishipa ya damu kama vile kuvimba kwa vena za miguuni (varicose veins)

Tiba ya kuongezeka unene kupita kiasi

Tiba ya tatizo hili ni mhusika kujitambua ya kwamba ana tatizo na kuwa tayari kupunguza uzito. Mabadiliko ya tabia ya mhusika ni muhimu sana, mabidiliko haya yawe ndio mfumo wa maisha yake ya kila siku.

Kupungua uzito na kujilinda au kutunza uzito ulionao baada ya kupunguza uzito ni jambo la msingi sana na inahusisha mazoezi, chakula na madiliko ya tabia ya mtu.

  • Mabadiliko ya tabia - Hii inahusisha muhusika kupunguza kiwango cha chakula anachokula lakini kiwe chenye virutubisho vyote muhimu vya afya na kuongeza kiwango cha ufanyaji mazoezi.
  • Mazoezi - Mazoezi husaidia kupunguza uzito hasa kipindi cha miezi sita ya mwanzo na hutunza uzito uliokusudiwa kwa muda mrefu. Pia hupunguza mafuta ya mwilini, huongeza ufanisi wa moyo, hupunguza tatizo la shinikizo la damu (hypertension), na kuweka sukari katika kiwango kinachohitajika mwilini.

Kama hujazoea kufanya mazoezi ni vizuri uanze taratibu na ujiwekee lengo kwa kufanya mazoezi kwa muda wa nusu saa kila siku, siku tano kwa wiki,(dakika 30 kila siku kwa siku tano kwa wiki). Mazoezi mazuri ni kama kuogelea, kuendesha baiskeli, kutembea, kunyanyua vitu vizito (visiwe vyenye uzito mkubwa), mazoezi ya viungo na kadhalika. Kama mtu ni mnene sana basi ni bora kuzungumza na daktari wako kabla ya kuanza mazoezi mapya. Baada ya kuanza mazoezi kwa mara ya kwanza, mwili utakuwa na maumivu, hii ni kawaida lakini kama mtu atapata maumivu zaidi ya masaa 2 baada ya kufanya mazoezi ni vizuri kumuona daktari.

  • Dawa - Zipo dawa nyingi za kupunguza uzito lakini ikumbukwe ya kwamba hakuna tiba ya tatizo hili na dawa hizi zina madhara mengi kama kuongeza shinikizo la damu (hypertension), matatizo ya moyo, kuharisha,msongo wa mawazo (depression) na mengineyo.
  • Chakula - Msingi wa kupunguza uzito au unene ni kujua ni kiwango gani cha calories mwili wako unahitaji kwa siku ili uwe unakula chakula ambacho hakitazidisha au kupunguza kiwango cha calories unazohitaji kwa siku. Mlo mzuri ni ule ulio na matunda kwa wingi, mboga za majani, nafaka ambazo hazijakobolewa, mafuta kidogo (less saturated fat). Vyakula vengine ni kama mayai, nyama isiokuwa ya mafuta (lean meat), samaki, kuku na vingineyo.
  • Tiba ya upasuaji - Kuna aina nyingi za upasuaji ambao unasaidia kupunguza uzito aina hizi ni kama gastric banding, gastric bypass (Roux-en-Y-procedure), liposuction. Kabla ya kufanyiwa upasuaji, muhusika atahitaji kupimwa kisaikolojia (psychological testing) na kupewa ushauri nasaha kwani tiba hii pia ina madhara yake.

Wanawake ambao wana uzito wa kupitiliza (obese women) wakiwa wajawazito wako kwenye hatari ya kupata madhara yafuatayo;

  • Kisukari cha mimba (Gestatitional diabetes) - kisukari hiki kinatokea wakati wa ujauzito na hupotea baada ya kujifungua mtoto.
  • Shinikizo la damu (hypertension)
  • Shinikizo la damu wakati wa ujauzito pamoja na kifafa cha mimba (pre-eclampsia & eclampsia)
  • Kuzaa kwa njia ya upasuaji (caesarean section)
  • Tatizo la kiumbe kutopata hewa vizuri wakati wa ujauzito (fetal distress)

Msongo wa mawazo kipindi cha ujauzito husababisha ulemavu kwa mtoto

$
0
0
stress in pregnant women

Watafiti wa magonjwa wanadai kuwa msongo mkali wa mawazo wakati wa ujauzito unaweza kusababisha hitilafu katika uumbaji wa mtoto na hatimaye mtoto kuzaliwa akiwa mlemavu.

Ripoti ya watafiti hao inazidi kuthibitisha matokeo ya tafiti zilizopita kuwa mama mwenye msongo wa mawazo wakati wa ujauzito kutokana na mambo kama kufukuzwa au kuachishwa kazi, kutengana na mwenza wake au kufiwa ana hatari ya kuzaa mtoto mwenye ulemavu kama vile midomo sungura (cleft lip na cleft palate) au matatizo kwenye uti wa mgongo (spina bifida).

Jopo la watafiti wa kidenmark likiongozwa na Dr Dorthe Hansen walifanya uchunguzi ili kuthibiitisha ukweli na uhakika wa dhana hii.

Wakitumia rikodi za taarifa za kitabibu za kipindi cha miaka 12 kutoka 1980 mpaka 1992 kutoka masjala ya Taifa ya kitabibu, watafiti hao waliweza kuwatambua wajawazito wote waliokumbwa na matatizo makubwa ya kimaisha wakati wa ujauzito na hata miezi 16 kabla ya kupata ujauzito. Matatizo makubwa ya kimaisha yaliyochunguzwa yalikuwa kukumbwa na msiba wa ndugu au jamaa wa karibu, ndugu au jamaa wa karibu kulazwa hospitali kwa mara ya kwanza baada ya kugundulika kuwa na kansa ya aina yeyote au ndugu au jamaa wa karibu kupatwa na ugonjwa wa mshtuko wa moyo. Mambo haya yalichunguzwa kwa kigezo kuwa, mjamzito yeyote aliyewahi kukumbana nayo ana hatari kubwa ya kuwa katika msongo wa mawazo bila kujali tabia yake, kama ana watu wa kumfariji au uwezo wake wa kukabiliana nayo.

Jopo hilo lilichunguza maendeleo ya mimba kwa wajawazito 3,560 ambao walikumbana na matukio hayo kwa kulinganisha na wajawazito wengine 20,299 ambao hawakukumbana na hali yeyote ambayo ingewasababishia kupata msongo wa mawazo wakati waujauzito.

Matokeo ya uchunguzi wao yalionesha kuwa ulemavu na hitilafu za viungo kwa watoto waliozaliwa ulikuwa mara mbili miongoni mwa kundi la wajawazito waliokumbwa na msongo mkali wa mawazo ikilinganishwa na kundi la kinamama ambao hawakuwa na hali hiyo.

Kadhalika ilionekana kuwa wanawake waliowahi kukumbwa na hali kama hiyo katika ujauzito mbili mfululizo za nyuma walikuwa katika hatari kubwa zaidi ya kuzaa watoto wenye ulemavu wa viungo tofauti na wale waliowahi kupatwa na hali hiyo mara moja tu au wale ambao hawakupatwa kabisa.

Ilionekana pia kuwa tukio lililoongeza uwezekano wa mtoto kuzaliwa akiwa na ulemavu wa viungo ilikuwa ni iwapo mjamzito atafiwa na mtoto wake mwingine mkubwa wakati akiwa katika miezi mitatu ya mwanzo wa ujauzito wake huu wa sasa. Hatari ya kuzaa mtoto mlemavu iliongezeka iwapo kifo cha mtoto huyo mkubwa kingetokea bila kutarajiwa kwa mfano kwa ajali.

Watafiti wanasema kwamba, msongo mkali wa mawazo huchangia kuathiri uumbaji wa mtoto aliye tumboni kwa kusisimua uzalishaji wa homoni ya cortisone. Homoni hii husababisha ongezeko la kiwango cha sukari katika damu na upungufu wa usambazaji wa hewa safi ya oksijeni kwa mtoto, mambo ambayo husababisha kutokea kwa hitilafu katika uumbaji wa viungo vya mtoto hatimaye kusababisha ulemavu wa viungo vya mtoto.

Uwezekano mwingine ni kuwa msongo mkali wa mawazo humchochea mama mjamzito kutumia zaidi vileo vyenye alcohol na pia kula lishe duni hali ambayo huongeza madhara zaidi kwa kiumbe kilicho tumboni.

Hata hivyo Professor Peter Hepper wa Chuo Kikuu cha Queen's cha Belfast, anasema hakushangazwa na mtokeo ya utafiti huo.

Anasema kuwa, "tunafahamu msongo wa mawazo husababisha mabadiliko ya kifiziolojia katika mfumo wa mwili wa mjamzito, na hivyo hakuna sababu kwanini mabadiliko hayo yasimfikie pia mtoto aliye tumboni kupitia kondo la nyuma na kumuathiri. Matokeo haya yanazidi kuthibitisha kile tulichokuwa tukikifahamu tangu awali kuwa msongo wa mawazo wa muda mrefu kwa mwanamke una madhara makubwa kwa mendeleo ya uumbaji wa mtoto aliye tumboni na hivyo basi hakuna budi kufanyike kila njia kuwasaidia wajawazito walio katika hali hii ili waweze kujifungua watoto walio na afya njema na salama."

Kukosa Usingizi Husababisha Upungufu wa Homoni ya Testosterone

$
0
0
Kukosa Usingizi
Mnamo mwaka 2007, watafiti nchini Marekani walifanikiwa kutoa ripoti inayojaribu kuhusisha ukosefu wa usingizi na upungufu wa homoni ya testosterone miongoni mwa wanaume watu wazima.

Kwa kawaida kiwango cha homoni ya testosterone hupungua kadiri mwanaume anavyozidi kuwa mtu mzima, na kwa baadhi ya wanaume, kupungua huku kwa testosterone huweza kusababisha ulegevu wa mwili, kukosa hamu ya ngono na hata kuvunjika mifupa ya mwili.

Watafiti wanasema kuwa, wapo baadhi ya wanaume walio kwenye miaka 80 bado huweza kuwa na kiwango cha juu cha testosterone sawa na kile kinachopatikana kwa wanaume vijana. Hata hivyo sababu kubwa inayofanya kuwepo na utofauti katika viwango vya testosterone miongoni mwa rika hizo mbili bado hazieleweki sawasawa, ingawa watafiti wanasema kuwa ukosefu wa usingizi miongoni mwa watu wazima na wazee unaweza kuwa chanzo kimojawapo cha kuwepo kwa hali hiyo.

"Matokeo ya utafiti wetu yanaongeza uwezekano kuwa wanaume watu wazima na wazee ambao hupata muda mfupi sana wa kulala nyakati za usiku huwa na kiwango kidogo sana cha homoni ya testosterone wakati wa asubuhi," anasema mtafiti Plamen Penev, wa kutoka Chuo Kikuu cha Chicago, nchini Marekani.

Wakati wa utafiti, wataalamu waliofanya uchunguzi huo walipima kiwango cha homoni ya testosterone katika damu kila asubuhi cha wanaume watu wazima wenye umri kati ya miaka 64 na 74 waliojitolea kushiriki kwenye utafiti huo. Aidha, mtindo wao wa kulala pamoja na kupata usingizi pia vilichunguzwa kila siku kwa muda wa wiki nzima.

Matokeo ya uchunguzi huo yalionesha kuwa kiasi cha usingizi walicholala kilikuwa na uhusiano wa karibu sana na kiwango cha testosterone katika damu wakati wa asubuhi. Wale waliopata usingizi mzuri na kwa muda mrefu (walau saa nane) walikuwa na kiwango kikubwa cha testosterone wakati wale waliopata usingizi wa kubabaisha (saa nne) walikutwa na kiwango cha chini cha homoni hiyo. Wastani wa muda wa kulala ulikuwa masaa sita.

"Pamoja na kwamba matokeo ya utafiti huu yanaonesha kuwa urefu wa muda wa kulala wa mtu waweza kuwa kiashiria cha mabadiliko ya homoni katika mwili yanayohusiana na umri, matokeo ya utafiti huu yanatoa tu picha ya nini kinachotokea mwilini kama mtu asipopata usingizi wa kutosha. Hata hivyo, tafiti zaidi zinahitajika ili kuthibitisha umuhimu wa uhusiano kati ya usingizi na mabadiliko ya homoni katika mwili," anasema Dr. Penev.

Wataalamu wa masuala ya afya ya usingizi wanashauri watu wazima kupata wastani wa angalau saa saba mpaka nane za kulala kila usiku ili kuwa na afya bora. Ripoti kamili ya matokeo ya utafiti huu inapatikana katika toleo la mwezi April, 2007 la jarida la afya la Sleep.

Korodani Bandia Kutengeneza Shahawa

$
0
0
shahawa
Wanasayansi nchini Marekani wako mbioni kutengeneza korodani bandia (artificial testicle) zitakazokuwa zikitengeneza shahawa ili kusaidia wanaume wenye matatizo ya uzazi.

Timu ya wanasayansi katika jimbo la San Fransisco nchini Marekani chini ya Dk Paul Turek wamepewa ruhusa ya kuendelea na utafiti huu baada ya kuahidiwa kupewa pesa za kutosha kutekeleza mradi huu.

Kwa muda mrefu, wanasayansi wamejaribu kutengeneza seli za shahawa (Sperm Cells) bila mafanikio kwa vile wamefanikiwa kutengeneza robo tatu tu ya mchakato wa kupata shahawa kamili. Hii inatokana na mazingira maalum yanayopatikana katika korodani kuhitajika kukamilisha utengenezaji wa shahawa hizo. Mazingira hayo ya uhalisia ni tofauti na mazingira yoyote yale ya nje katika utengenezaji shahawa.
Korodani hizo zitakuwa katika umbo la duara (cylindrical shape) na zitakuwa na urefu wa inchi kadhaa na hazitahitaji kupachikwa kwenye mwili wa binadamu. Aidha kifaa hiki kitakuwa tofauti na korodani nyingine bandia ambazo huwekewa wanaume waliokosa korodani moja kutokana na sababu mbalimbali.Kwa kawaida korodani za namna hii huwa hazitengenezi shahawa kwa vile hujazwa maji maalum ya saline solution ili kutumika kama mapambo.
Ili kufanikisha hili, wanasayansi hao itabidi kubuni utaalamu wa kutengeneza chembechembe za shahawa na wamepanga kutumia seli za asili (human embryonic stem cells) zilizoongezewa jena (genes) ili kuzifanya kuwa seli zinazoweza kuzaa chembechembe za shahawa na hivyo kutumika katika njia za kutungisha mimba kwenye maabara zinazojulikana kama In Vitro Fertilization (IVF)
Wakati tafiti zimeonesha ya kwamba inawezekana kutibu panya dume mwenye matatizo ya uzazi kutoka katika seli zao za asili yaani embryonic stem cells, kwa binadamu tafiti hizi zimeshindwa kuzaa matunda yoyote yale mpaka sasa.
Kyle Orwig, Profesa wa masuala ya uzazi na magonjwa ya wanawake (Obstetrics and Gynecology) na sayansi ya uzazi (Reproductive Sciences) anasema “Ni mradi wa matumaini sana lakini nina wasiwasi kama utafanikiwa, ukifanikiwa itakuwa ni mafanikio makubwa sana katika sayansi ya tiba ya uzazi.” Kwa kawaida, shahawa hutengenezwa na kuhifadhiwa katika korodani za mwanaume.
Matatizo ya kushindwa kutungisha mimba kwa wanaume hutokana na hitilafu katika mfumo wa uzalishaji shahawa kwenye korodani unaosababishwa na magonjwa ya cystic fibrosis, matatizo ya jena (genetic defects), korodani ambazo hazijashuka katika sehemu sahihi (undescended testis), madhara katika korodani kama ajali na saratani ya kwenye korodani.

Dalili na Ishara za Ujauzito

$
0
0
Mstari wima mweusi hutokea tumboni kuanzia chini ya kitovu

Dalili za ujauzito hutofautiana kati ya mwanamke na mwanamke, ingawa kuchelewa au kukosa hedhi ni dalili moja muhimu sana

Ni muhimu kuzitambua na kuzifahamu dalili hizi kwa sababu zinaweza kusaidia kuelezea au kutofautisha matatizo mengine mbali ya ujauzito.

Hebu sasa tuangalie dalili na ishara za Ujauzito:

  • Kutokwa damu kidogo ukeni wakati kiumbe kikipandikizwa kwenye mfuko wa uzazi, ingawa siyo wanawake wote hupatwa na dalili hii
  • Kukosa hedhi, hii ni moja ya dalili kubwa za ujauzito
  • Maumivu ya matiti na kuvimba matiti (huweza kutokea kati ya wiki ya 1 hadi ya 2)
  • Uchovu, wanawake wengi hujihisi uchovu na hali ya kutopenda kufanya lolote.
  • Kupoteza ladha au kuhisi ladha ya chuma mdomoni
  • Kuongezeka kwa hisia ya harufu, kipindi cha ujauzito wanawake wengi huongezeka hisia ya harufu
  • Kichefuchefu na kutapika
  • Maumivu ya kichwa
  • Kizunguzungu
  • Kukojoa mara kwa mara (hasa kati ya wiki 6-8)
  • Kubadilika rangi kwa ngozi inayozunguka chuchu kuwa nyeusi
  • Kutamani baadhi ya vyakula na kuchukia vingine
  • Kupanuka kwa mfuko wa uzazi
  • Tumbo kujaa au kuvimbiwa
  • Kununa na kukasirika haraka
  • Kiungulila au kupata choo kigumu
  • Kolostramu kuanza kutoka kwenye matiti
  • Kuongezeka uzito
  • Kuweza kupapasa mtoto (palpation of the baby)
  • Kulainika na kuvimba kwa shingo ya uzazi (Hegars sign) - kuanzia wiki ya 6
  • Shingo ya uzazi kubadilika rangi kuwa ya samawati kutokana na msongamano wa damu katika mishipa ya vena. Ishara hii huitwa pia Chadwick's sign

Dalili nyingine ni pamoja na

  • Mstari wima mweusi hutokea tumboni kuanzia chini ya kitovu (linea nigra)
  • Mama kuhisi mtoto akicheza (kuanzia wiki ya 20)
  • Maumivu ya mgongo hasa mimba ikishakuwa kubwa.
  • Kipimo cha mimba kuwa chanya (positive).
  • Kusikia mapigo ya moyo ya mtoto
  • Mtoto kuonekana kwenye kipimo cha ultrasound

Kutoga Ulimi ama Mdomo

$
0
0
mouth piercing
tongue piercing
Katika zama hizi za utandawazi na muingiliano baina ya tamaduni zetu za asili na tamaduni za kimagharibi, imekuwa ni kawaida kwa vijana wa rika tofauti na jinsia zote kutoga ulimi, mdomo, kitovu ama kivimbe cha nyusi kwa sababu tofauti tofauti sana.

Hivyo basi, ni muhimu sana kufahama ukweli kuhusu faida ama hasara za kutoga ulimi ama mdomo kabla hujatekeleza azma yako ya kutoga viungo hivi vya mwili.

Kutoga Ulimi ama Mdomo kunaweza kukusababishia madhara yasiyotarajiwa

Matokeo mazuri zaidi ya kutoga ulimi ama mdomo ni kutokutokea kwa kidonda ama kivimbe, wakati matokeo mabaya kutokea kwa baadhi ya watu ni pamoja na kuvunjika kwa meno/jino, kuvuja kiasi kikubwa cha damu, ama maambukuzi ya bakteria kwenye kidonda. Kutoga ulimi hujumuisha kutumika kwa sindano inayopenyezwa katikati ulimi ili kupitisha na kuhifadhi kipini, ama ndoana ama hereni ya urembo. Kazi hii ya kutoga ulimi mara nyingi ganzi huwa haitumiki. Baada ya kutoga, kuvimba kwa ulimi na maumivu ya muda hutokea.

Madhara ya kutoga Ulimi

  • Kuvuja damu kiasi kidogo hutarajiwa, kuna hatari ya mishipa ya damu kuharibiwa wakati wa kutoga ulimi, hali inayoweza kusababisha kuvuja damu kwa kiasi kikubwa kuliko ilivyotarajiwa.
  • Ingawa kuvimba kwa ulimi kunatarajiwa baada ya kitendo cha kutoga ulimi, wakati mwingine ulimi huvimba kwa kiasi cha kuziba kwa njia ya hewa. Kuziba kwa njia ya hewa kunaweza kusababisha kifo.
  • Ikiwa fundi wako wa kutoga ulimi hana uzoefu wa kutosha kufanya kazi hiyo, anaweza kuharibu mishipa ya fahamu ya ulimi hivyo kuharibu uwezo wa ulimi kuhisi/kutambua hisia za joto,baridi ama ladha ya chakula na vinyaji, vile vile kuathiri mienendo ya viungo vya eneo la kinywa na uso. Kwani nyuma ya ulimi kuna mishipa ya fahamu,mishipa hii ikiharibiwa ulimi utapooza hivyo kusababisha ganzi la kudumu, kuathirika kwa uwezo kuongea na kushindwa kutambua ladha za chakula/vinywaji
  • Vilevile kutoga ulimi kunakuweka kwenye hatari ya kupata maambukizi kwenye ulimi hasa ikiwa hutaweza kutunza hali ya usafi wa kinywa na meno kila wakati, hivyo kusababisha wadudu jamii ya bakteria kupenya na kuingia ndani ya ulimi na kusababisha maambuzi kwenye ulimi.
  • Hali ya kutoga ulimi inapodumu kwa muda mrefu, inaweza kusababisha nyufa kwenye meno, ama kuvunjika kwa nyuso za jino/meno kwa sababu ya msuguano wa muda mrefu kati ya jino/meno na hereni/kipini ama ndoana ya chuma/plastiki iliyohifadhiwa kwenye ulimi kwa muda mrefu. Nyufa hizi kwenye meno, kwa kawaida husababisha maumivu makali ya jino/meno. Hivyo basi meno haya yenye nyufa yanaweza kutibiwa kwa kuvalishwa kofia “ dental crown”. Si kawaida kupata magonjwa ya fizi ama kuta za ndani za shavu ikiwa umetoga ulimi na unatunza afya ya kinywa na meno vizuri.

Kutoga Mdomo

Kutoga mdomo ni pale pete ya urembo inapovalishwa ama kuhifadhiwa ndani ya mdomo. Majeraha ya kutoga mdomo hupona haraka zaidi, hata hivyo unapaswa kutunza kidonda cha jeraha hili kwa umakini

mkubwa wakati wa kupona. Vyakula, vinywaji na moshi wa sigara vinapofikia kidonda hiki, vinaongeza hatari ya kupata maambukizi kwenye kidonda.

Kishikizo vishikizo vya pete hii ya urembo kinaweza kusababisha vidonda kwenye fizi ama kuharibu jino. Kwa baadhi ya watu, tiba ya kupandikiza fizi hutumika kurejesha fizi zilizoathirika. Kama ilivyo kwa kutoga ulimi, kutoga mdomo pia kunaweza kuathiri mshipa wa fahamu hivyo kuathiri mienendo ya misuli ya kwenye eneo la kinywa na mdomo.

Je, una mpango wa kutoga Ulimi ama Mdomo?

Ikiwa unapanga kutoga viungo hivi vya mwili, unashauriwa ufanye mambo yafuatayo yatakayo kuwezesha kupata huduma ambayo haita athiri afya yako:

  • Hakikisha ngariba mtoga ulimi ama mdomo sio tu ana uzoefu wa kutosha kwenye kazi anayofanya, bali pia anazingatia usafi kufanya kazi zake.
  • Nenda hospitali kupata ushauri tiba mara tu unapoona ama maumivu ni makali sana, kuvimba kwa ulimi ama damu zinavuja kwa muda mrefu (zaidi ya dakika 30) ama ikiwa jeraha linapata maambukizi ya bakteria.
  • Unapokuwa na hereni, pete ama ndoana ya urembo kwenye ulimi ama mdomoni, unashauriwa kumwona daktari wa kinywa na meno kila baada ya miezi sita (6). Daktari wa meno atafanya kazi ya kuhakiki ikiwa kidude kilichovalishwa kina madhara kwenye meno ama fizi, hivyo kudhibiti athari zinazoweza kutokea kwa kutoga ulimi ama mdomo.
  • Wana michezo wanashauriwa kutovaa hereni, pete ama ndoana ya urembo iliyopo kwenye ulimi ama mdomoni wanapokuwa mchezoni, kwani vyombo hivi vya urembo vinaweza kunasa kwenye ngozi bila kutarajia hivyo kusababisha madhara yasiyotarajiwa.

Upungufu wa Damu Kipindi cha Ujauzito

$
0
0

Upungufu wa damu (anaemia) hutafsiriwa kama kupungua kwa kiwango cha hemoglobin katika damu damu chini ya kiwango kinachokubalika kiafya. Kiwango cha kawaida cha haemoglobin (Hb) katika mwili wa binadamu ni kati ya gramu 12 mpaka 14 kwa kila mililita ya damu. Hata hivyo shirika la afya duniani (WHO) linatambua kiwango cha mpaka 11gm/mililita kuwa cha kawaida kwa mama mjamzito. Hivyo basi mjamzito mwenye kiwango chochote cha haemoglobin chini ya 11 gm/mililita hutafsiriwa kuwa na upungufu wa damu. Hata hivyo nchi nyingi hasa zinazoendelea hutambua kiwango cha mpaka gramu 10 kwa mililita kuwa ni upungufu wa damu kwa mjamzito.

Kwa mjamzito anayehudhuria kliniki kwa mara ya kwanza, upungufu wa damu kipindi cha ujauzito humaanisha kiwango cha hemoglobin chini ya <11.0 g/dL, na mimba inapofikisha wiki 28 upungufu wa damu hutambuliwa iwapo hemoglobin itashuka na kuwa chini ya 10.5 g/dL.
Kwa kuzingatia hilo, mama mjamzito hushauriwa kupima wingi wa damu siku anapohudhuria kliniki kwa mara ya kwanza na pindi mimba inapofikisha wiki 28.

Viwango vya Anaemia
Upungufu wa damu unaweza kugawanywa katika viwango vikuu vinne, yaani upungufu wa damu wa kawaida (mild anaemia) ambao ni kati ya 9-11 gm/ml, upungufu wa damu wa kati (moderate anaemia) ambao ni kati ya 7-9 gm/ml, upungufu wa damu mkali (severe anaemia) ambao ni kati ya 4-7 gm/ml na upungufu wa damu mkali zaidi (very severe anaemia) ambao ni chini ya 4gm/ml.

Mzunguko wa madini ya chuma mwilini
Kwa kawaida mwili wa mwanamke huifadhi gramu 3.5 mpaka 4.5 za madini ya chuma. Asilimia 75 huifadhiwa kama hemoglobin katika chembe damu nyekundu, asilimia 20 kama ferritin katika mifupa na asilimia 5 inayobaki huifadhiwa katika misuli na vimeng’enyo vingine vya mwili.
Wanawake wasio wajawazito hupoteza karibu gramu 1 za madini ya chuma kutoka katika seli za mwili zinazokufa kila siku na gramu 1 zaidi kila siku wanayokuwa kwenye hedhi.

Ukubwa wa tatizo
Upungufu wa damu kipindi cha ujauzito ni tatizo linalowakumba kina mama wajawazito wengi sana, siyo tu Tanzania bali nchi nyingi zinazoendelea. Inakisikiwa kuwa karibu theluthi moja ya wajawazito katika miezi mitatu ya mwisho ya ujauzito hukumbwa na tatizo hili.
Kwa mujibu wa WHO, inakadiriwa kuwa karibu asilimia 56 ya wajawazito huko kusini mashariki ya Asia hukumbwa na tatizo hili. Kwa hapa Tanzania, hakuna takwimu sahihi kuhusu tatizo hili. Sehemu nyingine duniani, inakadiriwa kuwa karibu asilimia 4-16 ya vifo vinavyotokana na ujauzito husababishwa na upungufu wa damu. Aidha upungufu wa damu wakati wa ujauzito huongeza uwezekano wa madhara kwa mtoto ikiwemo kifo.

Chanzo cha upungufu wa damu wakati wa ujauzito
Kipindi cha ujauzito huambatana na mabadiliko mbalimbali ya mwili. Moja ya mabadiliko hayo ni ongezeko la maji (plasma volume) katika mzunguko wa damu. Katika hali hii, pamoja na kwamba kiasi cha damu huonekana kuongezeka, kiwango cha hemoglobini hupungua mpaka kufikia 11.5mg/dl.
Karibu asilimia 85 ya anaemia wakati wa ujauzito husababishwa na upungufu wa madini ya chuma mwilini. Upungufu wa madini ya chuma unaweza kusababishwa na kula chakula chenye kiasi kidogo cha madini haya au mwili wa mjamzito kushindwa kutunza madini ya chuma ya kutosha kutokana na ama mimba zilizopita au kupoteza kiasi kingi wakati wa hedhi kabla ya kushika mimba.

Vyanzo vingine ni pamoja na
  • Upungufu wa folic acid
  • Ugonjwa wa sickle cell
  • Lishe duni kabla na wakati wa ujauzito
  • Kupoteza damu kwa sababu ya kuumia au kuwa na minyoo (hookworms)
  • Ugonjwa wa malaria wakati wa ujauzito
  • Ugonjwa wa chembe damu nyekundu ujulikanao kama beta thalassaemia. Ugonjwa huu huwapata zaidi watu wanaoishi Asia ya kusini, Ulaya ya kusini na Afrika.
  • Upungufu wa vitamin B12
  • Ugonjwa sugu wa kuvunjika chembe damu nyekundu (chronic haemolysis) kama vile ugonjwa kurithi wa chembe damu nyekundu (hereditary spherocytosis)
  • Ugonjwa wa kupoteza hemoglobin kupitia mkojo (paroxysmal nocturnal hemoglobinuria)
  • Saratani ya damu (leukemia)
  • Matatizo ya kupoteza damu kwenye njia ya chakula (gastrointestinal bleeding)
  • Matatizo katika utumbo hasa wakati wa ujauzito.
Vihatarishi vya tatizo hili
  • Masuala ya kijamii kama vile umri wa mjamzito, kiwango chake cha elimu na uelewa kuhusu afya yake, kama ana mwenza wa kumsaidia kiuchumi, makazi anayoishi vinaweza kuchangia mjamzito kupata upungufu wa damu
  • Vihatarishi vingine ni vile vinavyohusu masuala ya uzazi kama vile idadi ya mimba zilizotanguli (waliowahi kuzaa wana hatari ya kupata anaemia kuliko wanaopata mimba kwa mara ya kwanza), kuwa na mimba ya mapacha na kuwa na historia ya kuzaa mtoto njiti
  • Vihatarishi vingine vinahusu tabia za mjamzito kama vile uvutaji sigara, unywaji wa pombe na kutohudhuria kliniki wakati wa ujauzito
  • Pia kuwa na magonjwa kama vile kisukari, magonjwa ya figo, pamoja na shinikizo sugu la damu
Madhara ya upungufu wa damu kwa mama na mtoto
Sehemu nyingine duniani, inakadiriwa kuwa karibu asilimia 4-16 ya vifo vinavyotokana na ujauzito husababishwa na upungufu wa damu. Aidha upungufu wa damu wakati wa ujauzito huongeza uwezekano wa madhara kwa mama na mtoto ikiwemo kifo. Madhara haya ni pamoja na
  • Madhara kwa mama kipindi cha ujauzito: kukonda au kuongezeka uzito kwa kiasi kidogo sana, kuhisi uchungu kabla ya muda, kondo la nyuma kutunga pasipostahili, shinikizo la damu wakati wa ujauzito, na chupa kupasuka kabla ya wakati.
  • Madhara kwa mama wakati wa kujifungua: kupatwa na uchungu usioeleweka na usio wa kawaida, mtoto kuvuja damu ndani kwa ndani, kupatwa na shock, hatari ya ganzi (anesthesia risk) kwa anayefanyiwa upasuaji, na moyo kushindwa kufanya kazi.
  • Madhara kwa mama baada ya kujifungua: maambukizi baada ya kujifungua, kizazi kushindwa kurudi katika hali ya kawaida au damu kuganda kwenye mishipa.
  • Madhara kwa mimba na mtoto atakayezaliwa: Madhara ni pamoja na mtoto kuzaliwa njiti, mtoto kuzaliwa na uzito mdogo, mtoto kuwa na score ndogo (poor Apgar score), mtoto kuzaliwa akiwa amechoka (fetal distress), na upungufu wa damu kwa mtoto
Watoto wanaozaliwa wakiwa na upungufu wa damu hukua kwa tabu, huwa na maendeleo duni ya kiakili na kimatendo (poorer intellectual developmental milestones), uwezekano mkubwa wa kuwa na kasoro mwilini na hata kifo. Kasoro hizo ni pamoja na matatizo ya magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo (congenital heart diseases

Dalili
Mjamzito mwenye upungufu wa damu wa kawaida mara nyingi anaweza asioneshe dalili zozote. Hata hivyo iwapo upungufu ni mkubwa, dalili za awali ni pamoja na uchovu wa mara kwa mara na kupumua kwa shida, kukosa hamu ya kula, mapigo ya moyo kwenda kasi, na kuchafuka kwa tumbo.
Wakati wa uchunguzi mjamzito anaweza kuonekana mweupe kuliko kawaida hasa sehemu za viganjani, kucha za vidoleni, ulimi, au macho. Anaweza pia kuwa na dalili za kuvimba miguu.

Vipimo na uchunguzi
Uchunguzi wa upungufu wa damu hufanywa kuwa kupima kiasi cha haemoglobin pamoja kufanya kipimo kingine cha damu kijulikanacho kama peripheral smear.
Vipimo vingine vya maabara ni pamoja na kipimo cha kufahamu uwezo wa kuhifadhi madini ya chuma yaani total ironbinding capacity (TIBC), kiasi cha feritin katika damu, kiasi cha folic acid. Katika mazingira mengine kipimo cha kuchukua sehemu ya supu ya mifupa na kuichunguza maabara yaani bone marrow biopsy kinaweza kufanywa. Hata hivyo hivi si vipimo vinavyofanywa mara kwa mara.

Matibabu
Mama mjamzito huitaji miligramu 2 mpaka 4.8 za madini ya chuma kila siku. Ili aweze kupata kiasi hiki, inampasa kula kati ya miligramu 20 mpaka 48 za madini ya chuma. Kwa jamii ambayo upatikanaji wa vyakula vyenye madini hayo ni wa shida, suala hili linaweza kuwa gumu sana kutekelezeka, ndiyo maana Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeweka mpango maalum wa kuwapa wajawazito wanaohudhuria kliniki madini ya chuma na folic acid ili kufidia pengo hilo.
Vidonge vya madini ya chuma ni salama, nafuu na njia makini ya kuongeza na kurekebisha upungufu wa damu mwilini. Kwa wajawazito ambao hawawezi kunywa, kwa sababu yeyote ile, njia ya sindano inaweza pia kutumika.
Wajawazito wanashauriwa kutumia miligramu 60 za madini ya chuma (ferrous sulphate) na 500mg za folic acid kila siku, ambapo utaratibu huu huendelea kwa miezi mitatu mpaka sita ili kuongeza hifadhi ya madini ya chuma mwilini, hata kama kiwango kinachotakiwa kitakuwa kimefikiwa.

Utumiaji wa vidonge vya madini ya chuma na baadhi ya vyakula: Kuna baadhi ya vyakula kama vile chai ya rangi ambavyo vikiliwa wakati mjamzito amekunywa vidonge vya madini ya chuma vinaweza kupunguza unyonyaji wake katika utumbo. Kwa upande mwingine baadhi ya vyakula vyenye vitamini C kama vile matunda ya jamii ya machungwa huongeza uwezo wa utumbo kunyonya madini ya chuma mwilini.

Vyakula vya kuongeza damu: Pamoja na mkakati huo, wajawazito hushauriwa pia kula vyakula vyenye madini ya chuma kwa wingi kama vile nyama, maini, mayai, samaki, mimea jamii ya kunde, maharage makavu, mboga za majani, matembele, na mikate iliyoongezwa madini ya chuma.

Matibabu ya upungufu wa damu mkali kwa wajawazito walio katika wiki za mwisho (baada ya wiki ya 32): Wagonjwa wa kundi hili hutibiwa hospitali. Wengi wanaweza pia kuwa na dalili za matatizo ya moyo, hivyo wanapaswa kulazwa na kupumzika kitandani, na wakati fulani kuongezewa hewa ya oksijeni. Pamoja na kutibiwa matatizo ya moyo, huongezewa pia damu (packed red cells) kwa vile vidonge vya madini ya chuma havitafaa kurekebisha tatizo hili kwa haraka kabla ya muda wa kujifungua kufika.

Matibabu ya maradhi mengine: kwa mazingira yetu, magonjwa kama malaria na minyoo huchangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa upungufu wa damu kwa wajawazito, hivyo basi magonjwa haya hayana budi kutibiwa kikamilifu ili yasilete madhara kwa mjamzito. Wajawazito wanaoishi maeneo yenye malaria kwa wingi hupewa dawa za SP kwa ajili ya kuwalinda wasipatwe na ugonjwa huu. Pia dawa za minyoo za Albendazole au mebendazole hutolewa kwa wajawazito baada ya miezi mitatu ya mwanzo ili kuua minyoo. Ili kuzuia kujiridia kwa minyoo, wajawazito pia hushauriwa kuvaa viatu/kandambili kila wakati, na kuhakikisha miili na mazingira yao yapo safi.

Maambukizi ya Fangasi katika Sehemu za Siri (v.Candidiasis)

$
0
0
candidiasis
Kati ya maambukizi yanayowasumbua wanawake wengi duniani ni maambukizi ya fangasi. Inakisiwa asilimia 75 ya wanawake wote duniani hupata maambukizi haya katika kipindi cha uhai wao.
Maambukizi ya fangasi katika sehemu za siri za mwanamke husababishwa na uwepo wa fangasi wanaojulikana kitaalamu kama Candida albicans. Maambukizi haya pia hujulikana kama yeast infection au thrush. Fangasi hupatikana kama vimelea vya kawaida katika mdomo, mpira wa kupitisha chakula sehemu inayojulikana kama pharynx, katika kibofu cha mkojo, uume na hata kwenye uke.
Mfumo mzuri wa kinga wa mwili pamoja aina fulani za bakteria wanaoishi pamoja na fangasi hawa husaidia sana katika kuthibiti maambukizi yanayoyosababishwa na aina hi ya fangasi.
Nini hutokea?
Kwa kawaida, Candida albicans huishi kwenye uke na sehemu nyingine (kama zilivyoelezewa hapo juu) bila kusababisha madhara yoyote yale isipokuwa pale mazingira ya eneo husika yanapobadilika kama vile mabadiliko katika hali ya pH ya eneo husika (ifahamike ya kwamba pH ya kawaida ndani ya uke ni 4.0 - 4.5) au uwiano wake na vimelea (microorganisms) wengine unapoharibiwa kutokana na sababu mbalimbali kama vile matumizi ya madawa aina ya antibiotics, kupungua kwa kinga mwilini kutokana na magonjwa mbalimbali n.k.
Maambukizi haya ya fangasi yanaweza kugawanywa katika sehemu kuu mbili;
1. Maambukizi yasiyo makali yaani uncomplicated thrush: Katika kundi hili, mgonjwa hupatwa na maambukizi mara moja hadi nne kwa mwaka na dalili zake huwa si mbaya sana na maambukizi haya husababishwa na fangasi wa jamii hii ya Candida albicans.
2. Maambukizi makali yaani complicated thrush: Katika kundi hili, mgonjwa hupatwa na maambukizi zaidi ya mara nne kwa mwaka, dalili zake kuwa mbaya zaidi au kama maambukizi yatakuwa yametokea kipindi cha ujauzito, ugonjwa wa kisukari, upungufu wa kinga mwilini. Aina hii kusababishwa na vimelea vya aina nyingine tofauti na Candida albicans.

Vihatarishi

Watu walio katika hatari ya kupata maambukizi ya fangasi hawa ni wale wenye;
• Kutumia sana dawa aina ya detergents kwenye sehemu za siri au douches (vifaa vinavyotumiwa kusafishia uke kwa kutumia maji yaliyochanganywa na siki au antiseptic yoyote ile) kwa sababu hali husababisha kuharibika kwa uwiano wa fangasi na aina nyingine ya vinyemelezi kama bakteria aina ya lactobacilli
• Kutumia sana madawa aina ya antibiotics, steroids ambayo yana tabia ya kushusha kinga ya mwili
• Mabadiliko ya mfumo wa homoni mwilini ambayo husababisha mabadiliko katika s ehemu za siri na hivyo kufanya kuwepo kwa ukuaji wa kasi wa fangasi hawa
• Ujauzito (kutokana na kubadilika kwa mfumo wa homoni mwilini na kupungua kwa kinga ya mwili). Hata hivyo ieleweke hapa kuwa si kila mjamzito hupatwa na maambukizi haya.
• Matumizi ya dawa za kupanga uzazi (vidonge vya majira)
• Upungufu wa kinga mwilini kutokana na magonjwa sugu kama kisukari, saratani aina yoyote ile, ugonjwa aina ya mononucleosis na nk.

• Ugonjwa wa ukimwi (HIV/AIDS)
• Matibabu ya homoni (hormonal replacement therapy) kutokana na sababu mbalimbali
• Matibabu ya kusaidia kushika mimba kwa wale wenye matatizo ya uzazi (infertility treatment)
• Msongo wa mawazo (stress)
• Utapia mlo (malnutrition)
• Kuvaa nguo au mavazi yanayoleta joto sana sehemu za siri kwa muda mrefu kama nguo za kuogelea (swimwear), nguo za ndani (chupi) zilizotengenezwa kwa kitambaa aina ya nylon, nguo za ndani zinazobana sana nk.
• Kujamiana kwa njia ya kawaida mara tu baada ya kujamiana kupitia njia ya haja kubwa au matumizi ya vilainishi venye glycerin wakati wa kujamiana pia yamehusishwa na maambukizi haya.
• Kuvimba kwa tezi la koo (goiter)
• Saratani ya tezi la koo (thyroid cancer)
• Wanawake wenye umri wa miaka kati ya ishirini na thelathini wapo kwenye hatari kubwa ya kupata maambukizi haya wakati wale ambao wameshaacha kupata hedhi au wale ambao hawajaanza kupata hedhi kabisa hawako kwenye hatari kubwa.

Kwa wanaume vihatarishi vya maambukizi haya ni;

• Kujamiana na mwanamke mwenye tatizo hili au maambukizi haya
• Upungufu wa kinga mwilini
• Matumizi ya madawa aina ya antibiotics kwa muda mrefu bila ushauri wa daktari
• Magonjwa sugu kama kisukari, saratani ya aina yoyote ile na nk.

Dalili na viashiria kwa wanawake;

• Kuwashwa sehemu za siri (kwenye tupu ya mwanamke)
• Kuhisi kuwaka moto sehemu za siri (burning sensation)
• Kufanya kama vidonda katika sehemu za siri (soreness)
• Maumivu wakati wa kujamiana (superficial dyspareunia)
• Maumivu au usumbufu wakati wa kujisaidia haja ndogo (wakati mtu anakojoa)
• Kuvimba na kuwa rangi nyekundu kwa mdomo wa nje wa tupu ya mwanamke (labia minora)
• Kutokwa na uchafu wa rangi nyeupe au nyeupe kijivu, unaoweza kuwa mwepesi, majimaji au mzito na ambao umefanana na jibini (cottage cheese like discharge) wenye muonekano unaojulikana pia kama curd-like appearance. Kwa kawaida, uchafu huu haumbatani na harufu yoyote isipokuwa panapokuwa na tatizo la ziada kama ugonjwa wa zinaa aina ya Bacteria vaginosis. Uchafu huu unaotoka hapa unaweza kuenea kwenye maeneo mengine yaliyokaribu na tupu ya mwanamke kama kwenye mitoki (groin area) au perineum na kusababisha kuharibika kwa ngozi katika sehemu hizo.
Dalili na viashiria hivi huwa mbaya zaidi wakati mwanamke anapokaribia kupata hedhi.

Dalili na viashiria kwa wanaume ni;

• Kuwashwa sehemu za siri
• Kuvimba na kuwa rangi nyekundu kwenye ncha ya uume
• Kuwepo kwa uchafu wa rangi nyeupe (kama nilivyoeleza hapo juu) kwenye sehemu ya juu ya uume.
• Kuwa na vidonda vidogo kwenye uume (sore on the glans)
Hata hivyo, mara nyingi wanaume hawaoneshi dalili zozote zile, ni vizuri kwa mwanamke kumueleza mwenza wake pale anapopata maambukizi haya ili naye pia apate kutibiwa.

Vipimo vya uchunguzi

Kabla ya vipimo vya uchunguzi, ni muhimu kwa daktari kuchukua historia ya mgonjwa kwa usahihi kabisa. Vipimo vitahusisha;
1. Uchunguzi wa uke (
(PV exam)
– Daktari huvaa gloves, na kuzilainisha gloves hizi kwa jelly maalum, mgonjwa hulala kwenye kitanda na kutanua miguu yake ili njia itanuke na kumrahisishia daktari kumfanyia uchunguzi, wakati akiwa tayari, daktari ataingiza vidole vyake viwili (cha shahada na cha kati) ukeni kwa dhumuni la
i. Kuhisi kama kuna uvimbe wowote ndani ya tupu ya mwanamke
ii. Kuangalia kama anapata maumivu wakati wa kujamiana
iii. Kuangalia kama kuna uchafu wowote unaotoka, wingi wake, rangi yake, harufu yake, uzito wake (mwepesi, majimaji au mzito), na aina ya uchafu unaotoka kama ni sahihi kutokana na maelezo ya mgonjwa au ni tofauti
iv. Kuangalia kama sehemu ya siri ipo kawaida
v. Kuangalia kama kuna uvimbe wowote wa tezi za sehemu ya siri (mitoki)
vi. Kuangalia nywele za sehemu za siri zilivyo na jinsi zilivyokaa
vii. Kuangalia shingo ya kizazi, bartholin glands nk.
viii. Kuangalia sehemu ya haja kubwa kama kuna skin tags, bawasiri (haemorrhoids) nk.
ix. Kuangalia kwenye kinembe
kama kuna tatizo lolote lile.
Hayo ni baadhi tu ya malengo na faida za kipimo hiki kwa vile humuwezesha daktari kugundua tatizo au maradhi mengine ya ziada ambayo hayajaanza bado kuonesha dalili zake kwa mgonjwa au mgonjwa mwenyewe hafahamu kama hali aliyo nayo ni tatizo. Hata hivyo inashauriwa sana kabla ya kufanya kipimo hiki, daktari amjulishe mgonjwa aina ya kipimo, lengo lake na jinsi kitakavyofanyika ili kumuandaa mgonjwa kisaikolojia. Aidha ni muhimu pia kumtaarifu wakati anapoanza kuingiza vidole.
2. Kuchunguza uchafu unaotoka kwa kutumia hadubini (microscope). Mara tu baada ya kuchukua sehemu ya uchafu kwa kutumia swab, kipimo hicho humwagiwa tone la 10% potassium hydroxide ambayo huyeyusha chembechembe za ngozi na kubakisha seli za Candida albicans. Kuwepo kwa pseudohyphae (mfano wa aina fulani ya mizizi au miguu ya fangasi hawa) pamoja na budding yeast cells (yaani seli za fangasi zinazojigawa kwa ajili ya kuzaliana) ni uthibitisho wa maambukizi ya fangasi aina ya Candida albicans.
3. Kuchukua kipimo na kuotesha kwenye maabara ili kuangalia aina ya uoto huo kama ni wa fangasi aina ya Candida albicans, ama la.
4. Kipimo cha mkojo (Urinalysis)
5. Vipimo vingine hufanyika kulingana na dalili zinazoashiria uwepo wa magonjwa mengine kama vile ugonjwa wa kisukari, HIV/AIDS, ugonjwa wa kuvimba tezi la koo (goiter), saratani ya tezi koo (thyroid cancer) nk.
Matibabu
Matibabu ya fangasi huusisha dawa za kutibu fangasi (antifungal drugs) kama vile dawa za kupaka za topical Clotrimazole, topical Nystatin, Fluconazole au topical Ketoconazole.
Wagonjwa wenye maambukizi yasiyo makali yaani uncomplicated va#@ginal candidiasis wanaweza kutumia dawa za kupaka (cream) kutoka dawa za fangasi za jamii ya -azole kama vile Butoconozale, Miconazole, Clotricomazole nk. Dawa hizi hutumika kwa muda wa siku 3-7 kulingana na aina ya dawa. Mgonjwa anashauriwa kupaka dawa ndani ya uke pamoja na maeneo yote yanayozunguka sehemu hiyo. Jinsi ya kupaka dawa hizi ni kuanzia mbele kuelekea nyuma.
Aidha mgonjwa anaweza kupewa dawa za kutumbukiza ukeni ambayo atatumia kwa muda wa siku 3-14 kulingana na aina ya dawa. Dawa hizo ni pamoja na Miconazole, Tiaconazole, Terconazole, Nystatin nk. Kidonge cha kumeza aina ya fluconzole pia huweza kutolewa. Dawa hizi nilizotaja hapa juu zina kawaida ya kuharibu ubora wa mipira ya kondomu zilizotengenezwa na mpira aina ya latex (latex condoms) pamoja na vifaa vya upangaji uzazi aina ya diaphragms. Ni vizuri kwa daktari kabla ya kumpa mgonjwa dawa hizi kumfahamisha kwa ufasaha jinsi ya kuzitumia na tahadhari anayotakiwa mgonjwa kuchukua. Inashauriwa kama baada ya matumizi haya bado mgonjwa ana dalili za maambukizi au mgonjwa akapata tena maambukizi haya ndani ya miezi miwili baada ya matibabu ya awali, basi anashauriwa kwenda kumuona daktari ili apate matibabu zaidi.
Kwa wale wenye maambukizi makali yaani complicated v@ginal candidiasis, kabla ya kupewa tiba, ni muhimu kwanza kufanyiwa kipimo cha kuotesha sehemu ya uchafu unaootoka ukeni ili kuwa na uhakika kama kweli fangasi wanaosababisha maambukizi haya ni Candida albicans ama la, kwani fangasi aina ya Candida glabrata pia wanaweza kusababisha aina ya maambukizi haya na huwa siyo rahisi kutibika kwa kutumia matibabu ya kawaida ya kutibu fangasi pamoja na pia si rahisi kuonekana kwa kutumia hadubini (microscope).
Matibabu ya wagonjwa wenye aina hii ya fangasi hujumuisha matumizi ya dawa za kupaka au vidonge vya kuweka ukeni kwa muda mrefu yaani kwa muda wa siku saba hadi kumi na nne (7-14) au dawa aina ya fluconazole ambayo hutumika kila baada ya siku tatu (yaani siku ya 1, siku ya 4 na siku ya 7). Mara baada ya kumaliza tiba hii, mgonjwa hutakiwa kuendelea nayo mara moja kwa wiki kwa muda wa miezi sita. Ikiwa matibabu haya hayatasaidia basi mgonjwa anaweza kushauriwa kutumia mchanganyiko wa fluconazole pamoja na dawa ya kupaka ya Clotrimazole mara mbili au moja kwa wiki kulingana na dozi ya dawa, au fluconazole na dawa nyingine za kupaka kwa wakati mmoja.
Matibabu ya wagonjwa wenye maambukizi hatari sana yaani severe v@#ginal candidiasis ambayo kwa kawaida huambatana na dalili kama uke kuwa mwekundu sana, uke kuvimba, michubuko ya ngozi ya ukeni (excoriation) na kutokea kwa mifereji kama vidonda (fissure formation) huwa ni dawa zozote za kupaka zilizotajwa hapo juu kwa muda wa siku 7 mpaka 14 au dawa ya fluconazole ambayo hutolewa mara mbili, ambapo dozi ya pili hutolewa siku ya tatu baada ya kutolewa kwa dozi ya awali (second dose 72hrs after initial dose).
Matibabu ya maambukizi ya fangasi ambayo hayasababishwi na Candida albicans kwa mfano Candida glabrata nk ni matumizi ya dawa za kupaka jamii ya nonfluconazole azole groups kama vile Posaconazole, Voriconazole nk zitolewazo kwa muda wa siku 7 mpaka 14 pamoja na kidonge cha Boric acid kwa muda wa siku 14. Mtu mwenye maambukizi haya pia anashauriwa kuonana na daktari bingwa wa magonjwa ya akina mama.
Kwa vile maambukizi ya fangasi hutokea sana kwa wanawake wajawazito, hivyo basi wanashauriwa kutibiwa kwa kutumia dawa za kupaka tu kwa muda wa siku 7. Aidha dawa aina ya Itraconazole haipaswi kutumiwa na mwanamke mjazito au anayekusudia kushika mimba. Dawa ya Ketoconazole haipaswi kutolewa bila ushauri wa daktari kwani ina madhara ya kusababisha ugonjwa hatari wa Ini (Fulminant hepatitis). Usugu wa fangasi dhidi ya dawa za jamii ya azole groups hutokea baada ya matumizi ya dawa za vidonge (vya kumeza) za kutibu fangasi kwa muda mrefu.
Maambukizi ya fangasi pia huonekana sana kwa wagonjwa wenye Ukimwi. Tiba ya maambukizi haya ni sawa na tiba ya watu ambao hawana ugonjwa wa Ukimwi. Hata hivyo, kwa wale wagonjwa wa ukimwi ambao wamepata maambukizi ya fangasi mara kwa mara wanashauriwa kunywa dawa aina ya fluconzole mara moja kwa wiki kama kinga dhidi ya maambukizi haya au kama njia ya kupunguza fangasi hawa. Kadhalika dawa za kutibu fangasi aina ya Itraconazole, Voriconazole, Posaconazole huingiliana sana katika utendaji kazi na dawa za kurefusha maisha za ugonjwa wa Ukimwi (Antiretroviral drugs, ARVs) aina ya Protease Inhibitors, PIs (rotinavir nk.) na Nonnucleoside Reverse Trancriptase Inhibitors, NNRTI (maraviroc nk).
Wakati mwingine, maambukizi ya fangasi yanaweza kuambatana na magonjwa ya zinaa (Bacterial vaginosis nk), hivyo dawa zitatolewa kulingana na dalili na historia ya mgonjwa.
Kinga ya maambukizi ya fangasi
• Kuosha sehemu ya siri kwa kutumia kitambaa kisafi kila siku na kuosha kuanzia mbele kuelekea nyuma, epuka kurudia ukishafika nyuma.
• Epuka matumizi ya sabuni zenye manukato, bubble baths, v@#ginal deodorant products, feminine hygiene, na bath powder.
• Vaa chupi ambazo hazibani sana na zilizotengenezwa kwa kutumia pamba au hariri (silk), epuka synthetic underwear.
• Epuka mavazi yoyote ya kubana kama jeans za kubana nk.
• Badilisha nguo za ndani (chupi) kila zinapopata unyevunyevu.
• Fua chupi zako kwa maji yenye nyuzi joto 90 na kuendelea.
• Tumia pad wakati tu unapozihitaji (kama umeingia kwenye mzunguko wako wa hedhi)
• Kula mlo wenye virutubisho vyote kamili (balanced diet)
• Epuka kufanya mapenzi na mpenzi wako ambaye amepata maambukizi ya fangasi.
• Epuka kuoga maji moto sana (hot baths) tumia maji ya uvuguvugu, hii kwa wale ambao wanaishi kwenye ukanda wa joto (tropical climate).
• Matumizi ya vifaa vya ngono , vifaa vya upangaji uzazi (diaphragms, cervical caps) yanaweza kuleta kujirudia kwa maambukizi ya fangasi kama havitaoshwa na kukaushwa vizuri baada ya kutumiwa.
• Baadhi ya tafiti zilizofanyika, zimethibitisha ya kwamba unywaji wa maziwa ya mtindi (yoghurt) yenye live culture, husaidia kupunguza maambukizi ya fangasi.

Tatizo la Kuota Matiti kwa Wanaume na Watoto (Gynecomastia)

$
0
0
Matiti kwa Wanaume
Tatizo la kuota matiti kwa wanaume na watoto limekuwa kubwa sana katika dunia ya leo. Inawezekana kabisa wakati unatembea njiani ukaona wanaume au watoto wadogo wa kiume wakiwa na matiti makubwa ambapo watu wengi huchukulia kama ni kawaida. Kitaalamu gynecomastia ni kukuwa kuliko kawaida yake kwa tishu ya kwenye titi inayojulikana kama glandular tissue. Tatizo hili huonekana sana kwa watoto wachanga na wanaume waliokatika umri wa kubaleghe, lakini pia huonekana kwa watu wazima na wazee.

Ukubwa wa tatizo (epidemiology)
Asilimia 60-90 ya watoto wachanga wanapata tatizo hili la kukuwa kwa matiti kwa mpito linalojulikana kitaalamu kama transient gynecomastia kutokana na kuwepo kwa kichocheo cha aina ya estrogen kwa wingi wakati wa ujauzito wa mama.
Kati ya asilimia 4-69 ya vijana walio katika umri wa kubaleghe imeonekana wanapata tatizo hili kutokana na kuwepo kwa wingi kwa kimengenyo aina ya estradiol.Mara nyingi huonekana katika umri kati ya miaka 10-12 na hupotea taratibu ndani ya miezi 18, si kawaida yake kuonekana kwa vijana walio na umri ya zaidi ya miaka 17. Asilimia 24-65 ya watu wazima hupatwa na tatizo hili, hii hutokana na kubadilishwa kwa wingi kwa kichocheo aina ya testerone kuwa estradiol na kutolewa kwa uchache kwa kichocheo hiki cha testerone kutoka kwenye korodani zinazoanza kuzeeka..Ikumbukwe ya kwamba kichocheo hiki testerone hutengenezwa katika korodani za mwanamume.
Pathofiziolojia (Nini hutokea?)
Kuongezeka ukubwa wa matiti kwa wanaume hutokana na kuharibika kwa mfumo wa vichocheo unaojulikana kama estrogen-androgen balance na hivyo kusababisha estrogen kutolewa kwa wingi ama kuongezeka kwa msisimko (sensitivity) wa matiti kwa kiwango cha zaidi ya kawaida kwa kichocheo aina ya estrogen kilicho kwenye mzunguko wa damu.Estrogen husababisha chembechembe zinazojulikana kama ductal epithelia kuongezeka kwa wingi, kurefuka (ductal elongation) na kugawanyika, kuongezeka kwa chembechembe za mafuta (ductal fibroblasts) na kuongezeka kwa mfumo wa damu kwenye matiti (increase vascularity).Estrogen hutengenezwa kutoka kwenye vichocheo vya testerone na androgen kwa kutumia kimengenyo kinachojulikana kama aromatase.

Aina za gynecomastia
•Puffy nipples – Kuongezeka ukubwa wa chuchu za matiti kutokana na kuongezeka kwa tishu aina ya glandular tissue.
•Pure glandular gynecomastia – Huonekana sana kwa wale wanaofanya mazoezi ya kujenga mwili (bodybuilders), kutokana na matumizi ya dawa za kujenga mwili (anabolic steroids) ambazo zinakuwa na kiwango kikubwa cha kichocheo aina ya testerone, ambacho hubadilishwa kuwa estrogen. Kwa wanaume wembamba, tatizo hili hutokea kutokana na kuongezeka kwa breast tissue gland pamoja na kuwepo/kutokuwepo kwa tishu aina ya adipose tissue.
Ni nani aliyekatika hatari ya kupata tatizo hili?
•Wanaume walio na umri zaidi ya miaka 50.
•Wenye uzito uliopitiliza (Obesity)
•Unywaji pombe kupindukia
•Magonjwa sugu ya figo au ya Ini
•Kuwepo kwa historia ya tatizo hili katika familia.
Visababishi vya kukuwa kwa matiti kwa wanaume
•Pseudogynecomastia – Kuongezeka kwa tishu zinazozunguka chuchu za matiti na huambatana na kuwepo kwa wingi wa tishu aina ya adipose. Mazoezi na kula vyakula venye virutubisho sahihi huondosha tatizo hili.
•Unilateral/asymetrical gynecomastia – Ni kuongezeka kwa titi moja pekee au la upande mmoja wa mwili wa mwanamume kutokana na sababu mbalimbali. Titi la upande wa pili huwa kwenye umbile na saizi ya kawaida. Bilateral gynecomastia ni kuongezeka kwa matiti yote mawili.
•Hypogonadism – Kutofanya kazi kwa korodani vizuri na kuwa ndogo. Hii husababishwa na magonjwa mbalimbali kama klinifelter'rs syndrome, pitituary insuffiency na nk.
•Umri – Kuzeeka pia kumehusishwa kutokea kwa tatizo hili kutokana na kutolewa kwa uchache kwa kichocheo cha testerone na kuongezeka kwa juhudi za kutengeneza kwa wingi kwa kimengenyo aina ya estradiol kutoka kwenye kichocheo aina ya testerone. Pia mabadiliko ya mfumo mzima wa vichocheo mwilini hasa kwa wale wenye uzito uliopitiliza.
•Uzito uliopitiliza (Obesity) – Watu wenye uzito uliopitiliza hupatwa na tatizo hili kutokana na kuharibika kwa mfumo wa vichocheo mwilini na hivyo kuongezeka kwa kichocheo aina ya estrogen mwilini mwao na wakati huohuo kupungua kwa kichocheo kingine aina ya testerone.
•Saratani – Baadhi ya saratani kama saratani ya kwenye korodani, kwenye tezi lililojuu ya figo (adrenal gland), saratani ya tezi la kichwa (pitituary tumor), huharibu mfumo mzima wa vichocheo mwilini hasa wa kuweka sawa vichocheo kati ya uanaume na uanawake (male-female hormonal balance).
•Hyperthyroidism – Kukuwa kwa ukubwa wa tezi la koo (thyroid gland) na hivyo kutengeneza kwa wingi kichocheo aina ya thyroxine.
• Tatizo la figo kushindwa kufanya kazi (Renal/Kidney failure) - Nusu ya wagonjwa wote wanaotibiwa tatizo la figo kushindwa kufanya kazi kwa kutumia hemodialysis hupatwa na tatizo hili la kukuwa kwa matiti kutokana na kuharibika kwa mfumo wa vichocheo mwilini (hormonal imbalance).
•Matatizo ya Ini – Dawa za kutibu magonjwa ya kwenye Ini kama liver cirrhosis, liver failure husababisha kutokea kwa tatizo hili kutokana na kukosekana kwa uwiano sawa wa mfumo wa vichocheo mwilini.
•Utapia mlo, ukame – Utapia mlo, ukame au kujikondesha husababisha kupungua kwa kichocheo aina ya testerone na kuongezeka kwa kichocheo aina ya estrogen na hivyo kuharibu mfumo wa vichocheo mwilini. Hii hutokana na kukosekana kwa virutubisho sahihi mwilini ambavyo vingi husaidia kurekebisha mfumo wa vichocheo mwilini na hivyo kumuepusha mtu na magonjwa mbalimbali pamoja na tatizo hili.
•Madhara ya dawa za kurefusha maisha (Antiretroviral therapy) kwa wagonjwa wa ukimwi.
•Utumiaji wa madawa ya kulevya kama bangi/marijuana.
Vipimo vya Uchunguzi
Vipimo hivi vitafanywa kulingana na historia ya mgonjwa, dalili na viashiria vya mgonjwa baada ya kupimwa na daktari.
•Kipimo cha damu (Complete Blood Count) – Kuangalia wingi wake, aina mbalimbali za chembechembe za damu na uwepo wa maambukizi ya bakteria.
•X-ray ya matiti (Mammogram) – Hutumiwa kuangalia tishu za kawaida na zile ambazo si za kawaida zilizo kwenye matiti. Husaidia kugundua uwepo wa saratani, cysts, na calcifications kwenye matiti.
•Liver function test – Mjumuiko wa vipimo vya damu kuangalia aina mbalimbali za vichocheo na vimengenyo ili kuweza kutambua kama mgonjwa ana ugonjwa wowote ule wa Ini na chanzo chake, vipimo hivi huangalia albumin, Alanine transaminase (ALT), Aspartate transaminase (AST), Alkaline phosphatase (ALK), Total bilirubin (TBIL), Direct bilirubin (Conjugated Bilirubin), Gamma Glutamyl Transpeptidase (GGT), Lactate Dihydrogenase (LDH).
•Tumor markers – Kipimo cha damu cha kuangalia viashiria vya saratani ya korodani kama AFP alpha feto 1 protein, Beta-HCG, LDH.
•Kipimo cha damu cha kuangalia wingi wa kichocheo cha aina ya testerone (Total and Free Testerone) Hufanyika asubuhi ambapo kiwango cha testerone huwa juu. Kiwango cha kawaida cha kichocheo cha testerone ni 300 - 1000 ng/dl (Kiwango hiki hupungua kwa asilimia 13 wakati wa mchana).
•Kipimo cha damu cha kuangalia vichocheo vinavyoonekana kwenye ugonjwa wa kukua ukubwa wa tezi la koo ( hyperthyroidism) kama kichocheo aina ya Thyroid Stimulating Hormone (TSH) ambacho huwa katika kiwango kidogo wakati wa kuugua ugonjwa wa hyperthyroidism, hutolewa na tezi la kwenye kichwa aina ya pitituary gland, vichocheo vyengine aina ya anti-TSH receptor antibodies (kwa wenye ugonjwa wa Grave’s disease), anti-thyroid – peroxidase (kwa wenye ugonjwa wa Hashimoto’s disease), na pia kuangalia wingi wa vichocheo aina ya T3 na T4. Kipimo cha Thyroid Scintigraphy pia huweza kutumiwa kutofautisha kati ya ugonjwa wa hyperthyroidism na ugonjwa wa thyroiditis. Kipimo hiki hutumia madini ya mionzi ya iodine (Iodine-131 ama Iodine-123).
•Vipimo vya kuangalia kama figo zimeshindwa kufanya kazi vizuri kama;
a)Kipimo cha utendaji kazi wa figo (Renal function tests) ambacho husaidia kuchunguza kiwango cha urea (blood urea nitrogen (BUN) katika damu. Aidha husaidia pia kuchunguza ongezeko la kiwango cha creatinine katika damu.
b)Uchunguzi wa kiwango cha madini mbalimbali katika damu (blood electrolytes)
c)Kupima kiasi cha mkojo kinachotolewa na mgonjwa katika masaa 24
d)Uchunguzi wa mkojo (Urine analysis): Rangi ya mkojo, kiasi cha electrolytes, uwepo wa usaha au damu au casts.
e)Ultrasound ya figo na kibofu cha mkojo
f)Renal biopsy.
Tiba ya Gynecomastia
Kama nilivyosema hapo awali, tatizo hili kwa vijana waliokatika umri mdogo au wa kubaleghe hupotea lenyewe taratibu ndani ya miezi 18. Kwa mzazi unatakiwa usihofu, lakini kama litaonekana kwa mtoto zaidi ya miaka 17, basi hapa mzazi unatakiwa kuchukua hatua za haraka ambazo ni kumuona daktari ili aweze kukusaidia kwa ufasaha zaidi.
1.Tiba ya madawa
•Tiba ya kutumia vichocheo (Testerone Replacement Therapy) – Kichocheo aina ya testerone hutolewa kwa mgonjwa kwa njia ya mdomoni, kwenye dripu, au kipachiko (patch forms). Hii hutolewa kwa wagonjwa ambao hawawezi kutoa testerone kutoka kwenye korodani zao kutokana na kupata ajali, ugonjwa au wale ambao hawana korodani kutokana na sababu mbalimbali.
•Dawa aina ya Selective Estrogen Receptor Modulator (SERMs) kama Tamoxifen, raloxifen, husaidia kupunguza ukubwa (volume) wa matiti lakini haziondoi tishu zote kwa ujumla. Aina hii ya tiba hutumiwa kwa wale wenye tatizo sugu la gynecomastia au wale wenye kupata maumivu makali sana. Dawa hizi zina madhara na hivyo ni vizuri kutumia kwa maelekezo ya daktari.
•Dawa aina ya Aromatase Inhibitors kama anastrozole, hufanya kazi kwa kuzuia kimengenyo aina ya aromatase na hivyo kuzuia utengenezwaji wa kichocheo aina ya estrogen. Tafiti nyingi zilizofanywa zimeshindwa kutoa majibu ya uhakika juu ya matumizi ya dawa hizi katika kutibu tatizo hili la kukuwa kwa matiti kwa wanaume.
2.Tiba ya Upasuaji – Kwa wale wenye tatizo hili sugu, upasuaji wa kurekebisha matiti unaweza kufanyika. Hii humuongezea mwanamume hali ya kujiamini na hivyo kuwa katika hali nzuri kisaikolojia, na huongeza ufanisi wa maisha yake ya kila siku.
3.Kupunguza uzito kwa kufanya mazoezi mara kwa mara na kula mlo wenye virutubisho vyote muhimu.
4.Kutibu chanzo au magonjwa mbalimbali kama hyperthyroidism, ugonjwa wa figo kushindwa kufanya kazi, saratani mbalimbali na nk.
5.Kuacha kunywa pombe na matumizi ya madawa ya kulevya kama bangi/marijuana.
6.Daktari kumbadilishia mgonjwa dawa baada ya kuona dalili za tatizo hili kwa wale wenye kutumia dawa za kutibu ugonjwa wa Ini, dawa za kurefusha maisha. Kwa wagonjwa wa Ukimwi, ni vizuri kwa daktari kabla ya kumpa mgonjwa dawa, kumfanyia mgonjwa kipimo cha fasting lipid profile, ili uweze kutambua kama dawa unazotaka kumpa zitamletea madhara au la. Na inashauriwa kurudia kipimo hiki kati ya miezi 3 hadi 6 baada ya kuanza dawa hizi za kurefusha maisha au baada ya kumbadilishia mgonjwa dawa. Hata hivyo sio dawa zote za kurefusha maisha zilizo na madhara haya, kwani zipo nyingine zinazopunguza kiwango cha mafuta mwilini na kwenye tishu.
Madhara ya Gynecomastia
1.Uwepo wa tatizo hili kwa muda wa zaidi ya miezi 12 au mwaka mmoja, husababisha matiti kutengeneza makovu au kwa kitaalamu scarring/fibrosis na hivyo kufanya tiba kwa kutumia dawa kuwa ngumu sana.
2.Wanaume wenye tatizo hili wapo kwenye hatari zaidi ya mara tano ya kupata saratani ya matiti ikilinganishwa na wanaume ambao hawana tatizo hili.
3.Kuathirika kisaikolojia (kuona aibu, kutojiamini, kujihisi tofauti na wanaume wenzake). Hali hii inaweza hata kumfanya mtu kuishi maisha ya huzuni au kushindwa kujumuika na watu katika shughuli mbalimbali kama michezo na nk.

Kusinyaa/Kuziba kwa mrija wa mkojo (Urethral stricture)

$
0
0

Mrija wa mkojo (urethra) ni kiungo muhimu kinachotoa mkojo nje ya mwili kutoka kwenye kibofu. Mrija huu unaposinyaa au kuziba hufanya utokaji wa mkojo kuwa wa mashaka na maumivu makubwa. Kusinyaa/ Kuziba kwa mrija wa mkojo huitwa pia urethral stricture.

Visababishi na vihatarishi vya tatizo hili
Kusinyaa kwa mrija wa mkojo husababishwa na kovu linalotokea katika sehemu ya mrija baada ya mtu kuumia, kufanyiwa upasuaji au kupona magonjwa ya zinaa. Inaweza pia kusababishwa na uvimbe karibu na eneo la kinena unaokandamiza mrija.

Vihatarishi vya tatizo hili ni pamoja na:

  • Kuwa na historia ya kuugua magonjwa ya zinaa
  • kuwahi kuwekewa mipira ya mkojo au vifaa vya namna hiyo (catheter au cystoscope)
  • Kuvimba tezi dume (BPH) kwa wanaume
  • kuwa na historia ya kuumia au kupata majeraha maeneo ya kinena. Hii hutokea sana kwa wale wanaopata ajali wakiendesha baiskeli
  • Kupata maambukizi ya mara kwa mara ya mrija wa mkojo (urethritis)

Ni nadra sana kwa tatizo hili kutokea kwa wanawake. Aidha ni nadra pia kwa mtoto kuzaliwa akiwa na tatizo hili (congenital urethral stricture).

Dalili
Mtu mwenye tatizo hili anaweza kuwa na dalili zifuatazo,

  • Kutoa shahawa zilizochanganyika na damu
  • Kukojoa mkojo mweusi au uliochanganyika na damu
  • Kupungua kwa kiasi cha mkojo kinachotolewa
  • Kukojoa kwa shida
  • kutoa uchafu katika mrija wa mkojo
  • kukojoa mara kwa mara
  • Kushindwa kumaliza mkojo wote
  • Kushindwa kuhimili kutoka kwa mkojo (mkojo kujitokea wenyewe/kujikojolea)
  • Maumivu wakati wa kukojoa
  • Maumivu chini ya tumbo
  • Maumivu ya kinena
  • Mtiririko dhaifu wa mkojo (hutokea taratibu au ghafla)
  • Mkojo kutawanyika ovyo wakati wa kukojoa
  • Kuvimba uume

Uchunguzi
Daktari atakufanyia uchunguzi wa mwili na namna unavyokojoa. Uchunguzi wa mwili unaweza kuonesha:

  • Kupungua kwa mkondo wa mkojo
  • Uchafu kutoka katika mrija wa mkojo
  • Kibofu kilichojaa/kuvimba
  • Kuvimba kwa mitoki ya maeneo ya kinena
  • Tezi dume iliyovimba au yenye maumivu
  • Kuhisi kitu kigumu chini ya uume
  • Uume kuvimba au kuwa mwekundu

Hata hivyo, wakati mwingine uchunguzi unaweza usioneshe tatizo lolote lile.

Vipimo
Vipimo ni pamoja na:

  • Kipimo cha kuchunguza mrija pamoja na kibofu cha mkojo (cystoscopy)
  • Kuangalia kiasi cha mkojo kinachobaki katika kibofu baada ya kukojo (Post-void residual (PVR) volume)
  • X-ray ya mrija wa mkojo (Retrograde urethrogram)
  • Vipimo vya magonjwa ya zinaa
  • Uchunguzi wa mkojo (Urinalysis) pamoja na kuotesha mkojo (Urine culture)

Matibabu
Mrija unaweza kutanuliwa wakati wa kipimo cha cystoscopy na hiyo ikawa ndiyo mojawapo ya tiba.
Iwapo njia ya kutanua mrija haioneshi mafanikio sana, upasuaji unaweza kuhitajika. Upasuaji unategemea eneo lilipo tatizo na ukubwa wa tatizo. Kama tatizo ni dogo/fupi na lipo mbali na bawabu inayotenganisha mrija na kibofu cha mkojo, linaweza kutatuliwa kwa kukata kasehemu kalikoziba wakati wa kufanya cystoscopy au kwa kuweka kifaa maalum cha kuzibua na kutanua mrija.

Kama tatizo ni kubwa zaidi, upasuaji wa wazi wa eneo husika unaweza kufanyika. Upasuaji huu unajumisha kukata sehemu iliyoziba na kisha kukarabati sehemu hiyo.

Kwa mgonjwa ambaye amepata shida ya ghafla ya kushindwa kutoa mkojo (acute retention of urine), matibabu ya dharura ya kumuwekea catheter kupitia juu ya kinena (suprapubic catherization) hufanyika. Hii husaidia kibofu kutoa mkojo nje kupitia kwenye bomba lililowekwa chini ya tumbo.

Ifahamike kuwa mpaka sasa hakuna dawa ya tatizo hili zaidi ya njia za upasuaji na nyingine zilizoelezwa hapo juu.

Matarajio
Mara nyingi matibabu huleta matokeo mazuri na mgonjwa anaweza kuishi maisha yake kama kawaida. Hata hivyo wakati mwingine, mgonjwa anaweza kuhitaji matibabu ya mara kwa mara ili kuondoa sehemu ya kovu iliyopo katika mrija wa mkojo.

Madhara ya tatizo hili
Tatizo hili halina budi kutibiwa haraka maana kama likiachwa linaweza kusababisha kuziba kabisa kwa njia ya mkojo na kusababisha mkojo kujaa katika kibofu, hali ambayo, pamoja na kuleta maumivu makali kwa mgonjwa inaweza pia kusababisha figo kushindwa kufanya kazi (ARF).

Kinga
Ni muhimu kujikinga dhidi ya magonjwa ya zinaa kwa kufanya ngono salama au kuacha kabisa kufanya ngono. Aidha kuwa makini na kazi au mambo ambayo yanaweza kukusababishia kuumia maeneo ya kinena.

Kuoza kwa meno (Dental Caries) ni ugonjwa wa kuambukiza

$
0
0
kuoza meno
Miaka ya nyuma iliaminika kuwa ugonjwa wa kuoza kwa meno si wa kuambukiza; lakini tafiti nyingi zilizofanyika zimedhihirisha ni ugonjwa wa kuambukiza. Jino lililooza linaweza kuambukiza meno yaliyogusana nalo na pia mgonjwa aliyeoza meno au mwenye wadudu wanaosababisha kuoza kwa meno anaweza kuambukiza mwenzake/wenzake.

Wadudu wanaosababisha kuoza kwa meno ni sehemu ya wadudu wakazi kinywani (oral flora). Wadudu hawa hujishikiza kwenye meno na kufanya utando, wana uwezo wa kuchachua vyakula hasa vyenye asili ya sukari na kutoa tindikali. Ni tindikali hii ambayo huvuta madini kwenye meno na kuweka matobo. Utando huu wa wadudu kwenye jino moja unaweza kuwa na wadudu nusu bilioni, miongoni mwao wakiwemo jamii ya mutans streptococci ambao kimsingi ndiyo wasababishaji wakuu wa kuoza kwa meno. Wadudu wengine ni kama Lactobacillus na Actinomyces.

Jinsi wanavyoambukiza

Ndani ya jamii ya wadudu hawa ziko jamii zingine ndogondogo ambazo zinatofautiana kwa uwezo wa kuchachua vyakula na kutoa tindikali na hata uwezo wa kujishikiza kwenye meno. Kwa mtu mwenye wadudu wasio wakali anaweza kuambukizwa na mwenzake mwenye wadudu wakali na hivyo kuingia kwenye hatari zaidi ya kuoza meno. Tafiti zimeonesha wapenzi/wanandoa wanaweza kuambukizana kwa njia ya kubusiana. Watoto wanaochangia ice cream/ice water mashuleni pia wanaambukizana kwa njia hii. Tafiti pia zimeonesha wazazi wanaotafunia vyakula watoto wao kama sehemu ya kuvilainisha wanaweza kuwambukiza pia watoto wao.

Njia nyingine ni jino lililooza kuambukiza mengine yanayogusana nayo, tindikali inayozalishwa na wadudu katika jino lililooza inaweza kuathiri jino lililo jirani. Ndiyo maana inashauriwa ukiona jino limeanza kuoza muone mtaalamu akalitibu au akaling’oe kama halitibiki ili lisiambukize mengine.

Namna ya kujikinga

  • Njia muhimu ni kutembelea cliniki za meno angalau kila baada ya miezi sita
  • Kuzuia watoto kuchangia vyakula mudomoni
  • Kupima kuangalia kiwango na aina za bakiteria zilizi kwenye mate yake na kupata dawa ikibidi.
  • Kuhusu kubusiana sina la kusema

Magonjwa ya Moyo ya Kuzaliwa (Congenital Heart Diseases)

$
0
0
Magonjwa ya Moyo ya Kuzaliwa
Muundo ya moyo na mishipa ya damu ni mojawapo ya vinavyooathirika katika magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo. Vijusi(fetuses) kati ya 8 hadi 10 huathirika kwa kila 1000.

Magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo huweza kutoa dalili mara tu baada ya kuzaliwa, utotoni na wakati mwingine husubiri mpaka ukubwani.

Magonjwa ya Moyo ya Kuzaliwa husababishwa na nini?

Kwa wengi sababu huwa haijulikani. Ila huwa kuna vitu hatarishi ambavyo hupelekea kuongezeka kwa uwezekano wa kupata magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo, vitu hivyo hatarishi ni:

  • Matatizo ya kijenetekia utotoni kama Downs syndrome, Turner’s syndrome, Marfan syndrome,
  • Matumizi ya dawa ya kutibu chunusi (acne) aina ya retinoic acid, madawa ya kulevya na unywaji wa pombe wakati wa ujauzito
  • Maambukizi ya virusi vya Rubella (German measles) kipindi cha kwanza cha ujauzito (1st trimester)

Kuna aina mbili za magonjwa ya moyo ya kuzaliwa:

  1. Cyanotic
  2. Non-cyanotic

Cyanosis ni hali ya kuwa na rangi ya samawati (katika midomo,ulimi, ganja za mikono na miguuni) kutokana na kukosa oksijeni ya kutosha mwilini.

1. Cyanotic

Magonjwa ya moyo ya asili ambayo yanaangukia katika kundi hili ni pamoja na

  • Tetralogy of fallots
  • Transposition of great vessels
  • Tricuspid atresia
  • Total anomalous pulmonary venous return
  • Truncus arteriousus
  • Hypoplastic left heart
  • Pulmonary atresia
  • Ebstein anomaly

2.Non-cyanotic

Magonjwa ya moyo ya asili yaliyo kwenye kundi hili hujumuisha

  • Ventricular septal defect (tundu katika kuta za ventrikali)
  • Atrial septal defect (tundu katika kuta za atria)
  • Patents ductus arteriousus
  • Aortic stenosis
  • Pulmonic stenosis
  • Coarctation of the aorta
  • Atrioventricular canal (endocardial cushion defect)

Dalili za Magonjwa ya Moyo ya Kuzaliwa

Kwa ujumla, wagonjwa wa moyo wa asili huwa na dalili zifuatazo;

  • Kupumua kwa shida
  • Kushindwa kula vizuri
  • Matatizo ya ukuaji
  • Matatizo ya ukuaji wa misuli ya mikono na miguu
  • Maambukizi ya mfumo wa hewa
  • Cyanosis kwa aina ya kwanza(rangi ya samawati katika midomo,ulimi, viganja vya mikono na miguuni)
  • Ongezeko la sauti ya ziada katika sauti za moyo kutokana na tatizo (heart murmur)
  • Mabadiliko kwenye kucha hasa za vidole vya mikononi (digital clubbing)

Vipimo na Uchunguzi

Baadhi ya vipimo vinavyotumika kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa haya ni

  • Echocardiogram/transesophageal echocardiogram
  • Cardiac catheterization
  • Magnetic Resonance Imaging
  • Electrocardiogram
  • Chest x-ray

Matibabu

Matibabu hutegemea aina ya ugonjwa wa moyo wa kuzaliwa nao, hivyo hapa nitaelezea kwa kifupi ila, maelezo zaidi nitatoa katika makala zinazokuja za ugonjwa mmoja mmoja.

Aina nyingi za magonjwa haya huwa na madhara makubwa hivyo huhitaji upasuaji kurekebisha kasoro hizo, pamoja na matibabu ya dawa (diuretics ambazo husaidia kupunguza maji na chumvi mwilini, digoxin ambayo husaidia kuongeza nguvu katika mapigo ya moyo).

Vilevile kuna tiba nyengine ambayo badala ya upasuaji kitaalamu Transcatheter ambapo kifaa cha kufunga au kupachika huwekwa kwenye catheter maalumu ambayo hupita kwenye mishipa ya damu mpaka kwenye kasoro na kurekebisha kwa kuziba tundu nakadhalika.


Sababu za Watoto Wachanga Kulia Mara kwa Mara na Namna ya Kuwabembeleza

$
0
0
kulia mtoto
Ni kawaida kwa watoto kulia. Hata watoto wanaozaliwa na afya njema kabisa wanaweza kulia kwa jumla ya wastani wa kati ya saa moja mpaka matatu kwa siku. Kwa vile watoto hawawezi kujifanyia chochote wao wenyewe zaidi ya kutegemea wazazi, walezi ama watu wengine wanaowazunguka katika kuwapatia chakula, joto, na faraja, kilio ni njia ya mtoto ya kuwasilisha moja ya mahitaji hayo.

Kama mzazi mpya, wakati mwingine inakuwa vigumu kutambua mtoto wako anahitaji nini anapolia. Mzazi anaweza kuwa na maswali kadhaa kichwani mwake, je, mtoto ana njaa, anasikia baridi, ana kiu, anaumwa ama amechoka? Katika siku za mwanzo, hali ya namna hii inawawia vigumu wazazi wengi, wasijue nini la kufanya. Hata hivyo, kwa kadiri siku zinavyopita mzazi mpya ataweza kutambua kuwa kilio cha mtoto wake kinamaanisha anahitaji nini kutokana na mfumo wake wa kulia.

Kadiri watoto wanavyokua ndivyo ambavyo hujifunza hatua mbalimbali za kuwasiliana na wazazi ama walezi wao. Wanakuwa na namna nzuri ya kuwasiliana kwa mfano kwa macho, na kutoa sauti, na hata kutabasamu ambavyo vyote kwa pamoja hupunguza haja ya kulia.

Sababu zinazofanya watoto kulia

Tuangalie sababu kadhaa zinazosababisha mtoto kulia na nini anachotakiwa mzazi ama mlezi kufanya pindi mtoto anapolia.

1. Hitaji la chakula

Njaa ni mmoja ya sababu kubwa inayowafanya watoto wengi kulia. Uwezekano wa mtoto kulia unaendana sana na umri wa mtoto. Kadiri jinsi mtoto alivyo mdogo zaidi ndivyo uwezekano wa kulia sana pindi anapohisi njaa unavyokuwa mkubwa, isipokuwa katika siku mbili za mwanzo baada ya kuzaliwa ambapo watoto hula kwa kiasi kidogo sana. Kwa kawaida katika siku mbili za mwanzo tangu mtoto kuzaliwa, maziwa ya kujilimbikizia mapema sana yaani ‘colostrum’ huwa ni kidogo sana kwa mama walio wengi na huanza kuongezeka kuanzia siku ya tatu baada ya kujifungua. Pia tumbo la mtoto katika kipindi hiki huwa bado dogo sana na hivyo uwezo wake wa kuhifadhi maziwa anayonyonya huwa bado mdogo hali ambayo humfanya mtoto kujisikia njaa. Hivyo kama mtoto wako analia, uwezekano mkubwa ni kuwa ana njaa na hivyo mzazi unashauriwa kumnyonyesha. Inawezekana mtoto asiache kulia mara moja, lakini mama unashauriwa kuendelea kumnyonyesha taratibu na mtoto anaweza kuacha kulia kwa kadiri anavyoburudika na chakula na kuanza kushiba. Iwapo mama unadhani mtoto wako ameshiba lakini bado anaendelea kulia, inawezekana kuna sababu nyingine zaidi.

2. Hitaji la starehe

Baadhi ya watoto wanakuwa na hisia kali pindi vitu kama nguo inapoelekea kumbana sana au iwapo anahisi kuna kitu chochote ndani ya nguo yake kinachomsababishia maumivu. Wapo baadhi ya watoto ambao hawaoneshi kuhangaika pale nepi zinapokuwa zimelowa sababu ya mkojo au kinyesi, kwa vile baadhi yao huihisi joto na hivyo kupendezewa na hali hiyo, wakati watoto wengine hulia na kuhitaji kubadilishwa nguo walizovaa mara moja, hasa kama ngozi zao laini zinasumbuliwa. Ni vyema kwa mzazi ama mlezi kumchunguza mtoto wako kama amechafua nepi na kumbadilisha. Vilevile ni vyema kuangalia kama nguo alizovikwa hazibani na hakuna chochote ndani ya nguo kinachomletea maumivu.

3. Hitaji la kuwa na joto la wastani

Baadhi ya watoto hawapendi kubadilishwa nepi au kuogeshwa. Hawajazoea kuhisi hewa yenye joto tofauti juu ya ngozi zao. Wengi wao hupendelea sana kuwa na hali ya jotojoto lililohifadhiwa. Kwa hiyo ni vyema kumbadilisha mtoto nepi haraka ili kuweza hifadhi joto lake. Inashauriwa pia kutokumvalisha nguo nyingi zaidi ya mahitaji ili mtoto asije akahisi joto zaidi ya analolihitaji mwilini na hivyo kupelekea kuanza kulia.

Inashauriwa pia kutomfunika mtoto kwa mashuka au mablanketi mengi hasa wakati wa kumlaza. Kabla ya kuamua ni kiasi gani cha nguo unachohitaji kumfunika mtoto wakati wa kulala, ni vyema kuangalia kama mwili wa mtoto ni wa moto au baridi isivyo kawaida. Unaweza kufanya hivi kwa kuhisi joto la tumbo lake kwa kutumia kiganja chako. Iwapo mtoto ana joto sana, unashauriwa kupunguza idadi ya nguo za kumfunika vivyo hivyo iwapo unahisi mtoto ana baridi isivyo kawaida inashauriwa kuongeza idadi ya nguo za kumfunikia. Usipime joto la mwili wa mtoto kwa kutumia joto la mikono au miguu yake kwani si kitu cha uhakika na mara nyingi huleta matokeo yasiyo sahihi kwa vile ni kawaida ya mikono au miguu ya watoto kuwa ya baridi.

4. Hitaji la kushikwa ama kubebwa

Baadhi ya watoto wanahitaji kuwa karibu na wazazi wao kwa kubebwa na kubembelezwa. Watoto wakubwa wanapata faraja kwa kuwaona wazazi wao wakiwa karibu na kusikia sauti zao, lakini mara nyingi watoto wachanga wanahitaji kushikiliwa na kubembelezwa kwa faraja. Kama umemlisha mtoto wako na kumbadilisha nepi wakati mwingine mtoto anahitaji kubebwa pia.

Baadhi ya wazazi uhofia kuwa wanaweza kuwaharibu watoto wao kimakuzi pindi wanapowabeba sana. Hiyo si kweli hususani kwa miezi michache ya mwanzo tangu kuzaliwa kwa mtoto. Wakati baadhi ya watoto hawapendi kubebwa, wapo wengine ambao hutaka kubebwa karibu muda mwingi. Iwapo mtoto wako ni wa namna hiyo, unaweza kumbeba mgongoni au kwa jinsi yeyote ile ambayo itakuruhusu kuendelea na shughuli zako nyingine.

5. Hitaji la mapumziko

Ni rahisi kudhani kuwa mtoto atapata usingizi wakati wowote popote pale alipo. Hata hivyo, kwa baadhi ya watoto, hali kama za ujio wa wageni, kelele au hali ya fujo zinaweza kumfanya mtoto kusisimka na hivyo kuwa vigumu kwake kutulia. Watoto wachanga wanaweza kupata ugumu wa kukabiliana na mambo ya kusisimua sana kwa mfano vitu kama taa, kelele, au kubebwa kwa kupokezana kutoka kwa ndugu au mgeni mmoja mpaka mwingine hasa wanapokuja kumtembelea mama. Hali hii humfanya mtoto kushindwa kustahamili na hivyo kuzidiwa na hayo yote. Wazazi wengi wamegundua kwamba watoto wao hulia zaidi kuliko kawaida wakati ndugu au jamaa wakiwatembelea hususani nyakati za jioni. Kama hakuna sababu nyingine maalum inayopelekea mtoto wako kulia, yawezekana basi kilio chake kinasababishwa na uchovu. Mzazi ama mlezi anashauriwa kumpeleka mtoto sehemu tulivu iwe chumbani au sehemu nyingine ambapo patamwondolea hali ya kusisimuliwa na hivyo kumfanya aweze kuacha kulia na kupata usingizi.

6. Hitaji la kitu cha kumfanya mtoto ajisikie vizuri

Iwapo umemlisha mtoto wako na kuhakikisha kuwa yupo vizuri lakini akawa bado anaendelea kulia, mzazi ama mlezi unaweza kuwa na hofu kuwa mtoto ni mgonjwa au ana maumivu. Ni vigumu sana nyakati za mwanzo kwa mzazi kutambua kuwa mtoto wake analia kwa sababu ya kutokuwa na furaha au kuna kitu kinachomuumiza. Mtoto ambaye ni mgonjwa mara nyingi hutoa sauti ya kilio kilicho tofauti na sauti yake ya kawaida. Sauti hii inaweza kuwa ya haraka zaidi au kali sana. Vile vile kwa mtoto ambaye amezoea kulia mara kwa mara, pindi anapoonesha hali ya utulivu isiyo ya kawaida inaweza kuwa dalili ya kwamba ni mgonjwa. Jambo muhimu la kukumbuka ni kwamba hakuna mtu anayemjua mtoto wako vizuri zaidi kuliko wewe. Kwa hiyo basi kama mzazi ama mlezi unahisi kwamba kuna kitu tofauti kwa mtoto wako ni vyema ukaonana na wataalimu wa afya. Wataalamu wa afya daima watayachunguza matatizo ya mtoto wako kwa umakini mkubwa na hivyo kujua sababu ya mtoto kulia. Mzazi ama mlezi unashauriwa kuonana na daktari iwapo mtoto wako ana shida ya kupumua pindi anapolia, au kama kulia kwa mtoto kunaambatana na kutapika, kuharisha ama kutopata choo.

7. Mtoto anahitaji kitu, lakini hujui ni nini

Wakati mwingine unaweza kushindwa kufahamu ni nini kinachomsababishia mtoto wako kulia. Wakati mwingine watoto wanakosa furaha. Hali hii ya kukosa furaha bila sababu inaweza kudumu dakika chache au saa kadhaa ambapo mtoto huendelea tu kulia mara kwa mara. Wakati mwingine baadhi ya watoto hulia kwa muda mrefu huku wakirusha rusha miguu. Hii hali yaweza kusababishwa na maumivu ayapatayo mtoto kwenye tumbo. Kwa kitaalamu hali hii hujulikana kama colic. Huwawia vigumu sana wazazi wengi kukabiliana na mtoto ambaye ana colic. Hakuna tiba ya uchawi kwa colic, aidha ni mara chache sana hali hii inadumu kwa zaidi ya miezi mitatu. Hata hivyo ni vyema kupata ushauri wa daktari pindi unapohisi mtoto wako ana colic.

Je, nini cha kufanya mtoto anapolia?

Kuna vitu ambavyo mzazi unaweza kufanya ili kumpa faraja mtoto wako pindi anapolia. Yawezekana baadhi ya mambo yatakayoshauriwa hapa yasiwasaidie watoto wote, hivyo basi mzazi ama mlezi ni vizuri ukamjua mtoto wako na kufahamu kwa undani ni kitu gani hasa kinachoweza kusaidia kumtuliza.

1. Kumbeba mtoto

Watoto wachanga huonyesha upendeleo fulani wa hisia, kama vile walivyokuwa ndani ya tumbo, hivyo basi unaweza kujaribu kumvingirisha mtoto wako katika blanketi au nguo zozote za kumbebea kama khanga au vitenge ili kuona kama atapenda hali hiyo. Watoto wengine hawapendi kuvingirishwa kwenye blanketi na hupenda aina nyingine ya kupata faraja kama vile kubebwa. Wapo wazazi wanaopenda kumbeba mtoto kiasi cha kumfanya mtoto asikie mapigo ya moyo, kitendo ambacho humpa faraja sana mtoto.

2. Kumwimbia nyimbo au sauti za kumbembeleza

Akiwa tumboni mwa mama, mara kwa mara mtoto alikuwa akisikia mapigo ya moyo ya mama. Hali hii ndiyo sababu kubwa ya watoto wengi kupendelea kubebwa na mama zao. Hata hivyo kuna aina nyingine za sauti zinazoweza pia kusaidia kumtuliza mtoto. Mzazi ama mlezi unaweza kujaribu kuweka muziki wa taratibu au kumuimbia mtoto nyimbo za kubembeleza kwa sauti ya chini sana. Unashauriwa kutokuweka miziki ya haraka au yenye sauti kubwa kwa sababu inaweza kumwondolea hali yake ya utulivu na hivyo kumfanya ashindwe kuacha kulia.

3. Jaribu kumkanda au kumsugua taratibu (masaji)

Kumkanda kanda au kumsugua mtoto taratibu mgongoni au tumboni kunaweza kumsaidia sana kumfariji mtoto. Iwapo inaonekana mtoto anapata tabu wakati wa kubeua au kucheua, jaribu kumlisha akiwa wima zaidi na kila baada ya kumlisha mweke juu ya bega lako na kumsugua taratibu mgongoni ili kumsaidia atoe gesi kwa kubeua. Baadhi ya watoto ambao wana “colic” wakati mwingine hutulia hasa wanaposuguliwa taratibu tumboni na hii huweza kuwafanya wajisikie vizuri kwa vile huihisi kwamba angalau mzazi ama mlezi unajitahidi kufanya kitu fulani kusaidia kumwondolea shida yake.

4. Mpatie kitu cha kunyonya

Kwa baadhi ya watoto waliozaliwa, haja ya kunyonya ni kubwa sana na hivyo kumpatia chuchu safi iliyotengenezwa kwa ajili hiyo au kidole kisafi cha mama inaweza kuleta faraja kubwa kwao. Kunyonya kutamsababishia mapigo ya moyo wake kuwa katika kiwango chake cha kawaida, kupumzisha tumbo lake, na kutulia.

Ulezi wa watoto wachanga ni kitu kigumu lakini ulezi wa mtoto ambaye hulia mara kwa mara ni ngumu zaidi. Kupata msaada na kuungwa mkono wakati unapohitaji msaada ni muhimu zaidi. Mzazi hana budi kufahamu kuwa kwa jinsi siku zinavyopita, na kwa kadri mtoto anavyokua, mtoto anajifunza njia mpya ya kuwa na uwezo wa kuwasilisha mahitaji yake na hivyo ni muhimu mzazi naye kujifunza njia hizo ili kumuwezesha kumpatia mtoto mahitaji yake anayohitaji kwa haraka na wakati unaostahili.
Viewing all 28 articles
Browse latest View live




Latest Images